Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kusamehe

Jinsi ya Kusamehe

KIKWAZO

Wewe na mwenzi wako mnapogombana, mnataja tena orodha ya makosa ya wakati uliopita, mnakumbushana mambo mabaya mliyotendeana zamani ambayo yalipaswa kusuluhishwa muda mrefu uliopita. Tatizo ni nini? Huenda mmoja wenu au nyote wawili hamjui jinsi ya kusamehe.

Mnaweza kujifunza kusameheana. Hata hivyo, kwanza, fikiria kwa nini huenda mume na mke wakaona ni vigumu kusameheana.

KWA NINI HILI HUTUKIA?

Mamlaka. Waume na wake fulani huamua kutosamehe ili wawe na kiasi fulani cha mamlaka juu ya wenzi wao. Halafu, wanapogombana, wanatumia matukio ya wakati uliopita kuwadhibiti wenzi wao.

Kinyongo. Mtu anapokosewa anaweza kuendelea kukumbuka jambo hilo kwa muda mrefu. Huenda mwenzi wa ndoa akasema ‘nimekusamehe’ lakini bado afungie kinyongo—na labda hata apange kulipiza kisasi.

Kukatishwa tamaa. Watu fulani huingia katika ndoa wakiamini kabisa kwamba maisha yao yatakuwa ya raha mustarehe. Kwa hiyo, kutoelewana kunapotokea, wanajiuliza inawezekanaje kwamba mwenzi waliyefikiri anawafaa kabisa ana maoni tofauti na yao. Matarajio yasiyo halisi yanaweza kumfanya mtu awe na kawaida ya kutafuta makosa na asiwe tayari kusamehe.

Kutoelewa kusudi la kusamehe. Watu wengi hukataa kuwasamehe wenzi wao kwa sababu hawaelewi kusudi la kusamehe. Kwa mfano, wao hujiambia:

Nikimsamehe, nitakuwa nikipunguza uzito wa kosa.

Nikimsamehe, lazima nisahau alichotenda.

Nikimsamehe, atanitendea vibaya hata zaidi.

Kwa kweli, kusamehe hakumaanishi mambo yatakuwa kama yalivyotajwa hapo juu. Hata hivyo, bado inaweza kuwa vigumu kusamehe—hasa kwa watu wenye uhusiano wa karibu kama mke na mume.

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Fahamu maana ya kusamehe. Katika Biblia, nyakati nyingine neno “samehe” linamaanisha “kuachilia.” Kwa hiyo, kusamehe hakumaanishi kwamba mara zote unapaswa kusahau mambo yaliyotokea au kupunguza uzito wa kosa. Nyakati nyingine kunaweza kumaanisha kuachilia mambo kwa manufaa yako na ya ndoa yako.

Tambua matokeo ya kutosamehe. Wataalamu fulani wanasema kwamba kuweka kinyongo kunaweza kusababisha matatizo ya kimwili na kihisia, yanayotia ndani kushuka moyo na kupanda kwa shinikizo la damu—isitoshe kunaweza kuharibu ndoa yako. Biblia ina sababu nzuri inaposema hivi: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari.”Waefeso 4:32.

Tambua faida za kusamehe. Roho ya kusamehe inawasaidia watu waliofunga ndoa waamini kwamba mwenzi wao hakuwa na nia mbaya alipowakosea na hivyo kuepuka kuhesabu mabaya. Kufanya hivyo kutawasaidia kujenga mazingira yanayozuia chuki na kuruhusu upendo kukua.Kanuni ya Biblia: Wakolosai 3:13.

Ona mambo kihalisi. Ni rahisi zaidi kusamehe ikiwa unamkubali mwenzi wako jinsi alivyo, licha ya upungufu wake. Kitabu Fighting for Your Marriage (Jinsi ya Kuiokoa Ndoa Yako) kinasema kwamba unapokazia fikira udhaifu wa mwenzi wako huenda ukasahau sifa zake nzuri. Kitabu hicho kinauliza hivi: “Ni nini hasa ambacho ungependa kukazia fikira kwa kuwa tayari umefunga ndoa?” Kumbuka, hakuna mtu mkamilifu—kutia ndani wewe.Kanuni ya Biblia: Yakobo 3:2.

Uwe mwenye kukubali sababu. Wakati ujao unapokasirishwa na jambo fulani ambalo mwenzi wako amesema au kufanya, jiulize hivi: ‘Je, kweli jambo hilo ni muhimu? Je, lazima niombwe msamaha, au naweza kupuuza kilichotokea na kusonga mbele?’Kanuni ya Biblia: 1 Petro 4:8.

Ikiwa ni lazima, zungumzieni jambo hilo. Eleza kwa utulivu jambo lililokukasirisha, na kwa nini unahisi hivyo. Usishuku kwamba mwenzi wako ana nia mbaya na usishikilie sana maoni yako, kwa kuwa kufanya hivyo kutamfanya tu mwenzi wako ajitetee. Badala yake, eleza tu jinsi matendo ya mwenzi wako yalivyokuathiri.