Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 BIBLIA INABADILI MAISHA

Niliishi Maisha ya Ubinafsi

Niliishi Maisha ya Ubinafsi
  • ALIZALIWA: 1951

  • NCHI: UJERUMANI

  • HISTORIA: NILIKUWA MWENYE KIBURI NA UBINAFSI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilipokuwa mchanga, familia yetu iliishi karibu na Leipzig, Ujerumani Mashariki, karibu na mpaka wa Cheki na Poland. Nikiwa na miaka sita, familia yetu ilihamia Brazili, kisha Ekuado kwa sababu ya kazi ya baba.

Nilipelekwa kwenye shule ya bweni nchini Ujerumani, nilipokuwa na umri wa miaka 14. Wazazi wangu waliishi mbali huko Amerika Kusini, hivyo nilihitaji kujitunza. Nikawa mwenye ubinafsi sana. Sikujali jinsi matendo yangu yalivyowaathiri wengine.

Wazazi wangu walirudi Ujerumani nilipokuwa na umri wa miaka 17. Mwanzoni, niliishi pamoja nao. Hata hivyo, kwa sababu ya ubinafsi, nilishindwa kuishi nao. Niliamua kuondoka nyumbani nilipokuwa na umri wa miaka 18.

Sikuwa nimetulia kwa sababu nilikuwa nikitafuta kusudi maishani. Baada ya kuchunguza mashirika mbalimbali na jinsi watu walivyoishi, niliamua kwamba jambo bora ambalo ningefanya maishani ni kutalii dunia hii maridadi kabla haijaharibiwa na wanadamu.

Niliondoka Ujerumani, nikanunua pikipiki, na kuelekea Afrika. Hata hivyo, baada ya muda mfupi ilibidi nirudi Ulaya ili nirekebishe pikipiki yangu. Baada ya hapo nilienda kwenye ufuo fulani wa bahari nchini Ureno. Niliacha kutumia pikipiki yangu na badala yake nikaamua kusafiri baharini.

Nilijiunga na kikundi cha vijana ambao walikuwa wakijitayarisha kuvuka Bahari ya Atlantiki. Miongoni mwao nilikutana na Laurie aliyekuja kuwa mke wangu. Mwanzoni, tulitembelea visiwa vya Karibea. Kisha, baada ya kukaa Puerto Riko kwa muda mfupi, tukarudi Ulaya. Tulitamani kupata mashua ambayo tungeikarabati ili tuishi ndani yake. Lakini baada ya kutafuta kwa miezi mitatu tu, mpango wetu ulikatizwa. Niliandikishwa kwenye jeshi la Ujerumani.

Nilitumika kwenye jeshi la wanamaji la Ujerumani kwa miezi 15. Katika kipindi hicho, mimi na Laurie tulifunga  ndoa na tukajitayarisha ili kuendeleza mpango wetu wa kusafiri. Kabla sijaenda jeshini, tulikuwa tumenunua mashua ya kuokolea uhai. Nikiwa jeshini, tuliikarabati hatua kwa hatua ikawa mashua ndogo ya kusafiria. Tulipanga kuishi humo na kuendelea kutalii dunia hii maridadi. Baada ya kumaliza utumishi wangu jeshini lakini kabla ya kumaliza kukarabati mashua, tulitembelewa na Mashahidi wa Yehova na tukaanza kujifunza Biblia.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mwanzoni, nilidhani sikuhitaji kubadili sana maisha yangu. Nilikuwa nimefunga ndoa na mwanamke niliyeishi naye, na nilikuwa nimeacha kuvuta sigara. (Waefeso 5:5) Nilifikiri mpango wetu wa kutembea ulimwenguni pote ulikuwa mzuri kwani tungetumia muda mwingi kuchunguza uumbaji maridadi wa Mungu.

Hata hivyo, nilihitaji kufanya mabadiliko hasa katika utu wangu. Kwa sababu nilikuwa mwenye kiburi na mbinafsi sana, nilifikiria tu uwezo wangu na mambo niliyotimiza. Niliishi maisha ya ubinafsi.

Siku moja, nilisoma Mahubiri ya Yesu ya Mlimani yanayojulikana sana. (Mathayo, sura ya 5-7) Mwanzoni, sikuelewa yale ambayo Yesu alisema kuhusu kuwa na furaha. Kwa mfano, anasema kwamba wenye furaha ni wale walio na njaa na kiu. (Mathayo 5:6) Sikuelewa jinsi kuwa na uhitaji kungemfanya mtu awe na furaha. Nilipoendelea kujifunza, nilitambua kwamba sote tuna uhitaji wa kiroho lakini tunahitaji kukubali kwamba tunao ili tuutimize. Ni kama alivyosema Yesu: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Mathayo 5:3.

Tulianza kujifunza Biblia tukiwa Ujerumani, hata hivyo, mimi na Laurie tulihamia Ufaransa, kisha Italia. Kila mahali tulipoenda, tuliwapata Mashahidi wa Yehova. Nilivutiwa sana na umoja wao na jinsi walivyopendana. Niliona kwamba Mashahidi wa Yehova ni udugu wa ulimwenguni pote. (Yohana 13:34, 35) Baada ya muda, mimi na Laurie tukabatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.

Baada ya kubatizwa, niliendelea kufanya mabadiliko katika utu wangu. Mimi na Laurie tuliamua kusafiri kwenye pwani ya Afrika, kuvuka Bahari ya Atlantiki na kuingia Marekani. Tukiwa baharini, sisi wawili tu kwenye mashua ndogo iliyozungukwa na maelfu ya kilometa za maji, nilitambua kwamba mimi ni duni sana kwa kulinganishwa na Muumba wetu mtukufu. Nilikuwa na muda mwingi (sikufanya kazi yoyote baharini) hivyo niliutumia kusoma Biblia. Nilichochewa sana na masimulizi kuhusu maisha ya Yesu duniani. Akiwa mwanamume mkamilifu, alikuwa na uwezo mwingi sana, hata hivyo hakujivuna. Alitumia maisha yake kumtumikia Baba yake wa mbinguni bali si kujiletea sifa.

Niliona kwamba nilihitaji kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani

Nilipotafakari kuhusu mfano wa Yesu, niliona kwamba nilihitaji kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani badala ya mambo niliyotaka kufanya. (Mathayo 6:33) Tulipofika Marekani, tuliamua kuacha kusafiri na badala yake kukazia fikira ibada yetu.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Kwa vile nilikuwa mbinafsi sana, mara nyingi nilitilia shaka maamuzi niliyofanya. Hata hivyo, sasa ninaongozwa na chanzo cha hekima inayotegemeka. (Isaya 48:17, 18) Nimepata pia kusudi maishani ambalo sikuwa nalo, yaani, kumwabudu Mungu na kuwafundisha wengine kumhusu.

Kwa kutumia kanuni za Biblia, mimi na Laurie tumeimarisha sana ndoa yetu. Pia, tumebarikiwa na binti mrembo anayemjua na kumtumikia Yehova.

Si kwamba maisha yetu yamekuwa shwari sikuzote. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova, tumeazimia kutovunjika moyo na kuendelea kumtegemea.—Methali 3:5, 6.