Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?

Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?

“NILIHISI kusongwa sana nizuie hisia zangu,” aeleza Mike alipokumbuka kifo cha baba yake. Kwa Mike, kuzuia huzuni yake lilikuwa jambo la kiume kufanya. Hata hivyo baadaye aling’amua kwamba alikuwa amekosea. Kwa hiyo rafikiye Mike alipofiwa na babu yake, Mike alijua jambo la kufanya. Yeye asema hivi: “Miaka michache iliyopita, ningalimpigapiga begani na kusema ‘Uwe mwanamume.’ Sasa niligusa mkono wake na kusema, ‘Hisi vile utakavyo kuhisi. Hilo litakusaidia ushughulike vya kufaa na hali hii. Ikiwa wataka niende, nitaenda. Ikiwa wataka nikae, nitakaa. Lakini usiogope kuhisi.’”

MaryAnne pia alihisi kusongwa azuie hisia zake wakati mume wake alipokufa. “Nilihangaikia sana kuwekea wengine kielelezo chema,” yeye akumbuka, “hivi kwamba sikujiruhusu nionyeshe hisia za kawaida. Lakini hatimaye nilijifunza kwamba kujaribu kuwa nguzo ya imara kwa ajili ya wengine hakukuwa kunanisaidia. Nilianza kuchanganua hali yangu na kusema, ‘Lia ikiwa ni lazima ulie. Usijaribu kuwa imara mno. Onyesha hisia zako zote kabisa.’”

Kwa hiyo Mike na pia MaryAnne wanapendekeza hivi: Jiruhusu uhuzunike! Nao wasema kweli. Kwa nini? Kwa sababu kuhuzunika ni ondoleo la kihisiamoyo linalohitajika. Kuondosha hisia zako kwaweza kutuliza ule msongo unaokabili. Wonyesho wa asili wa hisiamoyo, pamoja na uelewevu na habari sahihi, unakuruhusu uzionyeshe hisia zako ifaavyo.

Bila shaka, si kila mtu aonyeshaye huzuni kwa njia ileile. Na mambo kama ya kwamba mpendwa alikufa ghafula au kwamba kifo kilikuja baada ya ugonjwa wa muda mrefu huenda yakaathiri itikio la kihisiamoyo la wale wanaobaki. Lakini kuna jambo moja lionekanalo kuwa hakika: Kuzuia hisia zako kwaweza kukudhuru kimwili na kihisiamoyo pia. Ni bora zaidi kwa afya ukiondosha huzuni yako. Jinsi gani? Maandiko yana shauri lenye kutumika.

Kuondosha Huzuni​—Jinsi Gani?

Kuongea kwaweza kuwa njia yenye kusaidia kuondosha huzuni. Baada ya kifo cha watoto wake wote kumi, pamoja na misiba mingine ya kibinafsi, Ayubu yule mzee wa ukoo wa kale alisema hivi: “Hakika nafsi yangu yahisi kukirihi kuelekea maisha yangu. Nitatoa [Kiebrania, “nitaachilia”] hangaiko langu kuhusu mwenyewe. Nitasema katika uchungu wa nafsi yangu!” (Ayubu 1:2, 18, 19; 10:1, NW) Ayubu hakuweza tena kuzuia hangaiko lake. Alilazimika kuliachilia; alihitaji ‘kunena.’ Vivyo hivyo, mtunga-drama Mwingereza Shakespeare aliandika hivi katika drama iitwayo Macbeth: “Onyesha majonzi; huzuni isiyosema manong’ono hulemea moyo nayo huupasua.”

Kwa hiyo kuongea juu ya hisia zako pamoja na “rafiki wa kweli” atakayesikiliza kwa saburi na kwa kusikitikia kwaweza kuleta kadiri fulani ya kitulizo. (Mithali 17:17, NW) Mara nyingi kueleza maono na hisia hufanya iwe rahisi zaidi kuzielewa na kushughulika nazo kwa kufaa. Na ikiwa msikilizaji ni mtu mwingine aliyefiwa ambaye ameshughulika vya kufaa na hasara yake mwenyewe kwa mafanikio, huenda ukapata madokezo yenye kutumika juu ya jinsi ya kushughulika vya kufaa na hali yako. Mtoto wake alipokufa, mama mmoja alieleza kwa nini ilisaidia kuongea na mwanamke mwingine aliyekuwa amepatwa na hasara hiyohiyo: “Kujua kwamba mtu mwingine alikuwa amepatwa na jambo lilo hilo, alikuwa angali na afya nzuri ya kiakili na ya kihisiamoyo, na kwamba alikuwa angali anaendelea kuishi na kuwa na utaratibu fulani maishani mwake tena kuliniimarisha sana.”

Vielelezo vya Biblia huonyesha kwamba kuandika hisia zako kwaweza kukusaidia uonyeshe huzuni yako

Namna gani ikiwa huhisi starehe kuongea juu ya hisia zako? Baada ya kifo cha Sauli na Yonathani, Daudi alitunga wimbo wa maombolezo ambao katika huo alimwaga huzuni yake yote. Hatimaye wimbo huo wa maombolezo ukawa sehemu ya maandishi ya kitabu cha Biblia cha Samweli wa Pili. (2 Samweli 1:17-27; 2 Mambo ya Nyakati 35:25) Vivyo hivyo, wengine huona ni rahisi zaidi kujieleza kwa kuandika. Mjane mmoja aliripoti kwamba yeye alikuwa akiandika hisia zake kisha siku kadhaa baadaye alikuwa akisoma yale aliyokuwa ameandika. Aliona hiyo kuwa njia yenye kusaidia kuondosha huzuni.

Iwe ni kwa kuongea au kwa kuandika, kuwasilisha hisia zako kwaweza kukusaidia uondoshe huzuni yako. Kwaweza pia kuondolea mbali kutoelewana. Mama mmoja aliyefiwa aeleza hivi: “Mume wangu nami tulisikia juu ya waume na wake wengine waliotalikana baada ya kufiwa na mtoto, nasi hatukutaka hilo litupate. Kwa hiyo wakati wowote tulipokasirika, tukitaka kulaumiana, tulikuwa tukiongea juu yalo. Nafikiri tulikaribiana sana kwa kufanya hivyo.” Hivyo, kujulisha hisia zenu kwaweza kuwasaidia mwelewe kwamba hata ingawa huenda ikawa mnashiriki pamoja hasara ile ile, wengine waweza kuhuzunika kwa njia tofauti—kwa mwendo wao wenyewe na kwa njia yao wenyewe.

Jambo jingine liwezalo kurahisisha ondoleo la huzuni ni kulia. Kuna “wakati wa kulia,” Biblia husema. (Mhubiri 3:1, 4, NW) Kwa hakika kifo cha mtu fulani tumpendaye huleta wakati wa jinsi hiyo. Kulia machozi ya huzuni kwaonekana kuwa sehemu ya lazima ya kawaida ya kupona.

Mwanamke mmoja mchanga aeleza jinsi rafiki wa karibu alivyomsaidia ashughulike vya kufaa na hali wakati mama yake alipokufa. Yeye akumbuka hivi: “Sikuzote rafiki yangu alikuwapo kwa ajili yangu. Alilia pamoja nami. Aliongea nami. Niliweza tu kuonyesha hisiamoyo zangu waziwazi sana, na hilo lilikuwa jambo la maana kwangu. Sikuhitaji kuaibika kwa sababu ya kulia.” (Ona Warumi 12:15.) Wewe pia hupaswi kuaibika kwa sababu ya machozi yako. Kama vile tumeona, Biblia imejaa vielelezo vya wanaume na wanawake wa imani—kutia na Yesu Kristo—waliolia machozi ya huzuni waziwazi bila kuonekana kuwa na aibu.—Mwanzo 50:3; 2 Samweli 1:11, 12; Yohana 11:33, 35.

Katika kila utamaduni, watu wanaohuzunika huthamini kupokea faraja

Huenda ukaona kwamba kwa wakati fulani hisiamoyo zako zitatokea bila kutazamiwa. Huenda machozi yakatiririka bila ya wewe kujua kimbele. Mjane mmoja aliona kwamba kununua vitu kwenye duka kubwa (jambo alilokuwa amefanya mara nyingi pamoja na mume wake) kuliweza kumfanya alie, hasa wakati, kwa sababu ya kuzoea, alipofikia ili achukue vyakula vilivyopendwa sana na mume wake. Jionyeshe saburi. Na usihisi kwamba ni lazima uyazuie machozi yasitoke. Kumbuka, hiyo ni sehemu ya asili na ya lazima ya kuhuzunika.

Kushughulika vya Kufaa na Hali ya Kuhisi Una Hatia

Kama ilivyoonyeshwa kimbele, wengine wana hisia za kuwa na hatia baada ya kufiwa na mpendwa. Hilo huenda likasaidia kueleza sababu ya ile huzuni nyingi ya yule mwanamume mwaminifu Yakobo alipofanywa aamini kwamba mwana wake Yusufu alikuwa ameuawa na “hayawani-mwitu mkali.” Yakobo mwenyewe alikuwa amemtuma Yusufu aende akachunguze hali njema ya ndugu zake. Kwa hiyo yaelekea Yakobo alisumbuliwa na hisia za kuwa na hatia, kama vile ‘Kwa nini nilimtuma Yusufu akiwa peke yake? Kwa nini nilimtuma kwenye eneo ambalo limejaa mahayawani-mwitu?’—Mwanzo 37:33-35, NW.

Labda wewe wahisi kwamba uzembe fulani upande wako ulichangia kifo cha mpendwa wako. Kung’amua kwamba kuhisi una hatia—iliyo halisi au ya kuwaziwa tu—ni itikio la kawaida la huzuni kwenyewe kwaweza kusaidia. Hapa tena, usihisi kwamba hupaswi kuonyesha hisia hizo. Kuongea juu ya jinsi uhisivyo kwamba una hatia kwaweza kuandaa ondoleo kubwa linalohitajiwa la huzuni.

Ingawa hivyo, ng’amua kwamba haidhuru ni kadiri gani tumpendavyo mtu mwingine, sisi hatuwezi kudhibiti maisha yake, wala hatuwezi kuzuia “wakati na tukio lisilotazamiwa” lisiwapate wale tuwapendao. (Mhubiri 9:11, NW) Ingawaje, bila shaka madhumuni yako hayakuwa mabaya. Kwa kielelezo, kwa kutofanya mpango wa kumwona daktari mapema zaidi, je, wewe ulikusudia mpendwa wako awe mgonjwa na kufa? Bila shaka sivyo! Basi, je, una hatia kwelikweli ya kusababisha kifo cha mtu huyo? La.

Mama mmoja alijifunza kushughulika vya kufaa na hali ya kuhisi ana hatia baada ya binti yake kufa katika aksidenti ya gari. Yeye aeleza hivi: “Nilihisi nina hatia kwa sababu ya kumtuma. Lakini nikaja kung’amua kwamba kuhisi hivyo lilikuwa jambo la upuuzi. Kumtuma aende na baba yake afanye kazi fulani hakukuwa kosa. Hiyo ilikuwa aksidenti tu iliyo mbaya sana.”

‘Lakini kuna mambo mengi sana ambayo laiti ningalisema au kufanya,’ huenda ukasema. Ni kweli, lakini ni nani kati yetu awezaye kusema kwamba sisi tumekuwa baba, mama, au mtoto mkamilifu? Biblia hutukumbusha hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2; Warumi 5:12, NW) Kwa hiyo kubali uhakika wa kwamba wewe si mkamilifu. Kuendelea kufikiri-fikiri ati “laiti tu ningalifanya hivi au vile” hakutabadili chochote, lakini huenda kwaweza kukawiza kupata kwako nafuu.

Ikiwa una sababu nzuri za kuamini kwamba hatia yako ni halisi, isiyowaziwa tu, basi fikiria lile jambo la maana zaidi ya yote katika kutuliza hisia ya kuwa na hatia—msamaha wa Mungu. Biblia hututia moyo hivi: “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha.” (Zaburi 130:3, 4) Huwezi kurudia wakati uliopita na kubadili chochote. Lakini, waweza kumwomba Mungu msamaha kwa makosa ya wakati uliopita. Kisha nini? Ikiwa Mungu anaahidi kufuta kabisa makosa yako, je, wewe hupaswi pia kujisamehe?—Mithali 28:13; 1 Yohana 1:9.

Kushughulika vya Kufaa na Kasirani

Je! wahisi kasirani pia, labda kuelekea madaktari, wauguzi, marafiki, au hata yule mfu? Ng’amua kwamba hilo pia ni itikio la kawaida la kufiwa. Labda kasirani yako yaandamana kwa asili na uchungu unaohisi. Mwandikaji mmoja alisema: “Ni kwa kuja kutambua kukasirika kwako tu—si kwa kutenda kulingana nayo bali kwa kujua unahisi hivyo—ndipo uwezapo kuwa huru na matokeo yayo yenye uharibifu.”

Huenda pia ikasaidia kueleza au kushiriki kasirani hiyo na mwingine. Jinsi gani? Kwa hakika si kwa mifoko isiyodhibitiwa. Biblia huonya kwamba kasirani yenye kudumu muda mrefu ni hatari. (Mithali 14:29, 30) Lakini huenda ukapata faraja katika kuongea juu yayo pamoja na rafiki mwenye kuelewa. Na wengine huona kwamba mazoezi yenye nguvu wanapokuwa wamekasirika ni njia yenye kusaidia ya kuondosha kasirani.—Ona pia Waefeso 4:25, 26.

Ingawa ni jambo la maana kuonyesha hisia zako waziwazi na kwa haki, onyo lafaa kutolewa hapa. Kuna tofauti kubwa kati ya kuonyesha hisia zako na kuwafokea wengine. Hakuna haja ya kuwalaumu wengine kwa sababu ya kasirani na kukatishwa tamaa kwako. Kwa hiyo uwe mwangalifu juu ya kueleza hisia zako, lakini si kwa njia yenye uhasama. (Mithali 18:21) Kuna msaada mmoja muhimu sana katika kushughulika vya kufaa na huzuni, na tutauzungumzia sasa.

Msaada Kutoka kwa Mungu

Biblia hututia moyo hivi: “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:18) Ndiyo, zaidi ya jambo jingine lolote, uhusiano na Mungu waweza kukusaidia ushughulike vya kufaa na kifo cha mtu fulani umpendaye. Jinsi gani? Madokezo yote yenye kutumika ambayo yametolewa hadi sasa yametegemea au yanapatana na Neno la Mungu, Biblia. Kuzitumia kwaweza kukusaidia ushughulike vya kufaa na hali.

Kwa kuongezea, usipunguze umaana wa thamani ya sala. Biblia hutusihi hivi: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Ikiwa kumweleza rafiki mwenye kusikitikia hisia zako kwaweza kusaidia, basi kummwagia “Mungu wa faraja yote” yaliyomo moyoni mwako kwaweza kukusaidia hata zaidi kama nini!—2 Wakorintho 1:3NW.

Si kwamba sala hutufanya tuhisi vizuri zaidi tu. “Msikiaji wa sala” anaahidi kuwatolea roho takatifu watumishi wake waiombao kwa moyo mweupe. (Zaburi 65:2; Luka 11:13, NW) Na roho takatifu, au kani ya utendaji ya Mungu, yaweza kukupa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili uendelee kuishi siku moja baada ya nyingine. (2 Wakorintho 4:7, NW) Kumbuka: Mungu aweza kuwasaidia watumishi wake waaminifu wavumilie tatizo lolote lile ambalo huenda wakakabili.

Mwanamke mmoja aliyefiwa na mtoto wake akumbuka jinsi nguvu ya sala ilivyomsaidia yeye na mume wake wakati wa hasara yao. “Ikiwa tulikuwa nyumbani usiku na huzuni ikazidi, tulikuwa tukisali pamoja kwa sauti kubwa,” yeye aeleza. “Mara ya kwanza tulilazimika kufanya lolote bila yeye—mkutano wa kutaniko wa kwanza tuliokwenda, mkusanyiko wa kwanza tuliohudhuria—tulikuwa tukisali ili kupata imara. Tulipoamka asubuhi na ikaonekana hatuwezi kuvumilia uhalisi wa hali hiyo, tulikuwa tukisali kwa Yehova atusaidie. Kwa sababu fulani, nilikuwa na umivu kali kwelikweli la kimoyoni kuingia nyumbani nikiwa peke yangu. Kwa hiyo kila wakati nilipokuja nyumbani nikiwa peke yangu, nilikuwa tu nikimwomba Yehova tafadhali anisaidie kudumisha kadiri fulani ya utulivu.” Mwanamke huyo mwaminifu aamini kwa uthabiti na ifaavyo kwamba sala hizo zilifanya hali iwe tofauti. Wewe pia waweza kuona kwamba likiwa tokeo la sala zako zenye udumifu, ‘amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda moyo wako na nguvu zako za akili.’—Wafilipi 4:6, 7; Warumi 12:12NW.

Kwa kweli ule msaada ambao Mungu huandaa hufanya hali iwe tofauti. Mtume Mkristo Paulo alisema kwamba Mungu “hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tupate kuweza kufariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki.” Ni kweli, msaada wa kimungu hauondoi umivu, lakini waweza kufanya hali iwe rahisi zaidi kuvumilia. Hilo halimaanishi kwamba hutalia tena au utamsahau mpendwa wako. Lakini waweza kupata nafuu. Na upatapo nafuu, yale ambayo umepatwa nayo yaweza kukufanya uwe mwenye kuelewa na mwenye kusikitikia zaidi katika kuwasaidia wengine washughulike vya kufaa na hasara hiyohiyo.—2 Wakorintho 1:4NW.