Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Ulijua?

Je, Ulijua?

Sababu gani watenda-maovu waliouawa walivunjwa pia miguu?

Juu ya kuuawa kwa Yesu pamoja na watenda-maovu wawili kwenye miti ya mateso, habari ya Injili inasema hivi: ‘[Wayahudi] wakamuomba Pilato aagize miguu yao ivunjwe na miili iondolewe.’—Yohana 19:31.

Sheria ya Wayahudi ilisema kwamba mwili wa mutenda-maovu uliotundikwa juu ya muti kisha kuuawa kwake ‘usibaki usiku kucha juu ya muti.’ (Kumbukumbu la Torati 21:22, 23) Inawezekana Wayahudi walitumia sheria ileile kwa wale waliouawa na Waroma juu ya muti. Katika hali hiyo, kuvunja watu miguu kungefanya wakufe haraka ili wazikwe mbele ya Sabato iliyoanza kisha kushuka kwa jua.

Wahukumiwa wengi waliouawa namna hiyo walitundikwa juu ya muti kwa misumari iliyotoboa mikono na miguu yao. Wakati muti huo ulisimamishwa wima, mutu alibaki mwenye kuninginia akiwa na maumivu makali sana, kwa sababu uzito wote wa mwili wake ulikuwa juu ya misumari hiyo. Ili kupumua, iliomba mutu ajisindirie kwenye musumari, ao misumari, iliyokuwa katika miguu. Ikiwa mifupa ya miguu yake ilikuwa yenye kuvunjwa, haingewezekana afanye hivyo. Kwa hiyo, angekufa haraka kwa sababu ya kusongwa pumuzi ao kwa sababu ya maumivu.

Kombeo zilitumiwa namna gani katika vita wakati wa zamani?

Kombeo ndiyo silaha yenye Daudi alitumia ili kumuua Goliathi, aliyekuwa mutu murefu na munene sana. Inawezekana Daudi alijifunza kutumia silaha hiyo katika miaka yake ya ujana alipokuwa muchungaji.—1 Samweli 17:40-50.

Muchoro kwenye ubao unaoonyesha wapigaji wa kombeo waasiria wakishambulia muji wa wayahudi wenye nguvu sana

Michoro ya kombeo inaonyeshwa kati ya vitu vilivyotengenezwa na Wamisri na Waasiria katika nyakati za Biblia. Silaha hiyo ilitengenezwa kwa mufuko mudogo wa ngozi ao wa nguo ulio wazi wenye kufungwa juu ya kamba mbili. Mupigaji wa kombeo angetia katika mufuko wake jiwe lisilo na vikwaruzo ao la muviringo lililokuwa na ukubwa kama wa chungwa (ndimu-utamu) na ambalo labda lilikuwa na uzito wa gramu 250. Kisha alizungusha kombeo juu ya kichwa chake na kuachilia kamba moja, na kufanya jiwe liende kwa nguvu nyingi sana na kupiga bila kukosea mutu ao kitu kilichoviziwa.

Uchimbuaji katika eneo la Mashariki ya Kati ulifanya watu wapate majiwe mengi sana yaliyotumiwa katika kombeo kwenye vita wakati wa zamani. Labda wapiganaji wa vita wenye ufundi walitupa majiwe kwa mwendo wa kilometa 160 mupaka 240 kwa saa moja. Watu wenye elimu hawakubaliane ikiwa kombeo ilikuwa na uwezo wa upinde, lakini bila shaka kombeo ingeweza kutokeza hatari.—Waamuzi 20:16.