Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Njia za Kusuluhisha Malalamiko Yanayotokea Mara Nyingi

Njia za Kusuluhisha Malalamiko Yanayotokea Mara Nyingi

Njia za Kusuluhisha Malalamiko Yanayotokea Mara Nyingi

BIBLIA haisemi kuwa ndoa ni mpango rahisi. Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika kwamba wenzi wa ndoa wangelazimika kupambana na “matatizo ya kila siku.” (1 Wakorintho 7:28, Today’s English Version) Lakini mume na mke wanaweza kufanya mengi kupunguza matatizo yao na kuzidisha furaha ya mmoja na mwenzake. Fikiria malalamiko sita yafuatayo ambayo hutolewa mara nyingi na waume na wake mbalimbali, na uone jinsi kufuata kanuni za Biblia kunavyoweza kukusaidia.

1

LALAMIKO LA

“Mimi na mwenzi wangu wa ndoa tumeanza kutengana polepole.”

KANUNI YA BIBLIA:

“Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”WAFILIPI 1:10.

Ndoa yako ni moja kati ya mambo muhimu zaidi maishani mwako. Inahitaji kutangulizwa. Kwa hiyo, chunguza kama shughuli zako za kila siku zinachangia lalamiko hilo. Usiache shughuli hizo zikutenganishe na mume au mke wako. Bila shaka, kazi na hali nyingine zisizoepukika zinaweza kufanya wenzi wa ndoa wasikae pamoja kwa muda fulani. Lakini unaweza na unapaswa kuweka mipaka kuhusiana na jambo lolote ambalo una uwezo wa kuamua kulifanya au kutolifanya—kama wakati unaotumia pamoja na rafiki zako, au katika mambo ya kujifurahisha.

Hata hivyo, wenzi fulani wa ndoa wanaweza kuamua kufanya kazi ya ziada au kutumia wakati mwingi zaidi katika mambo ya kujifurahisha kusudi waepuke kutumia wakati pamoja na mwenzi wao wa ndoa. Watu kama hao ‘hawatengani’ na wenzi wao. Wanakimbia matatizo. Ikiwa mmoja wenu ana tabia kama hiyo, mnahitaji kuchunguza chanzo cha matatizo yenu na kuyatatua. Wewe na mwenzi wako wa ndoa mnaweza tu ‘kuwa mwili mmoja’ kikamili mkitumia wakati pamoja.—Mwanzo 2:24.

Jinsi ambavyo wengine wametumia shauri hilo: Andrew * na Tanji, ambao ni mume na mke kutoka Australia, walifunga ndoa miaka kumi iliyopita. Andrew anasema: “Nimetambua kuwa kufanya kazi kupita kiasi au kutumia wakati mwingi pamoja na marafiki ni jambo linaloweza kuathiri ndoa. Kwa hiyo, mimi na mke wangu hutenga wakati wa kuzungumza na kuelezana hisia zetu.”

Dave na Jane, ambao wanaishi Marekani, walifunga ndoa miaka 22 iliyopita, nao hutumia muda wa nusu saa kila jioni kuzungumzia matukio ya siku na mambo ya kibinafsi kabla ya kuanza shughuli zao za jioni. Jane anasema: “Huu ni wakati muhimu sana kwetu hivi kwamba haturuhusu chochote kituvuruge.”

2

LALAMIKO LA

“Sipati tena ninachotaka katika ndoa hii.”

KANUNI YA BIBLIA:

“Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.”1 WAKORINTHO 10:24.

Mtu anayefikiria tu faida anazoweza kupata katika ndoa, hataweza kamwe kupata furaha ya kweli, hata kama ataoa au kuolewa mara ngapi. Ndoa inafanikiwa ikiwa wenzi wote wawili wanazingatia zaidi kutoa kuliko kupokea. Yesu anataja sababu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Jinsi ambavyo wengine wametumia shauri hilo: Maria na Martin, ambao wanaishi Mexico, walifunga ndoa miaka 39 iliyopita. Lakini hali haijawa rahisi sikuzote. Wanakumbuka wakati fulani ambao ulikuwa mgumu sana. Maria anasema: “Tulikuwa tunabishana vikali, nami nikasema jambo fulani ambalo lilimvunjia Martin heshima kabisa. Alikasirika sana. Nilijaribu kumweleza kwamba sikumaanisha yale niliyosema, na kwamba nilikuwa nimekasirika tu. Lakini hakunisikiliza.” Martin anasema: “Wakati wa mabishano hayo, nilianza kuwaza kuwa hatuwezi kuishi pamoja tena, na kwamba nilipaswa tu kuacha kujaribu kufanikisha ndoa yetu.”

Martin alihitaji kuheshimiwa, naye Maria alitaka Martin amwelewe. Hakuna aliyepata alichotaka.

Walitatua tatizo lao jinsi gani? Martin anasema: “Nilingoja mpaka nilipotulia, kisha sote wawili tukaamua kufuata shauri la Biblia lenye hekima la kuwa wenye heshima na huruma. Tangu tufunge ndoa, tumejifunza kwamba hata matatizo yatokee mara nyingi kadiri gani, tunaweza kuyashinda iwapo tutamwomba Mungu atusaidie na iwapo tutafuata mashauri ya Biblia.”—Isaya 48:17, 18; Waefeso 4:31, 32.

3

LALAMIKO LA

“Mwenzi wangu wa ndoa hafanyi yale anayopaswa kufanya.”

KANUNI YA BIBLIA:

“Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.”WAROMA 14:12.

Bila shaka, ndoa haiwezi kufanikiwa sana ikiwa mwenzi mmoja tu ndiye anayejitahidi kuifanya ifanikiwe. Lakini hali itakuwa mbaya hata zaidi iwapo mume na mke watapuuza wajibu wao na kulaumiana.

Ikiwa wakati wote utafikiria yale ambayo mwenzi wako anapaswa kutimiza, hutakuwa mwenye furaha kamwe, na hasa ikiwa utatumia kasoro zake kuwa sababu ya kupuuza mambo unayopaswa kutimiza. Kwa upande mwingine, ukijitahidi kuwa mume au mke mwema, ndoa yako itakuwa bora. (1 Petro 3:1-3) Jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba unamthibitishia Mungu kuwa unaheshimu mpango wa ndoa, na jitihada zako zitamfurahisha sana.—1 Petro 2:19.

Jinsi ambavyo wengine wametumia shauri hilo: Kim na mume wake wanaoishi Korea, walifunga ndoa miaka 38 iliyopita. Kim anasema: “Wakati fulani, mume wangu hunikasirikia na kuacha kuzungumza nami, na hata sijui ni kwa nini. Hali hiyo hunifanya nihisi kwamba hanipendi tena. Nyakati nyingine mimi huwaza, ‘Kwa nini anataka nimwelewe, hali yeye hajaribu kuelewa jinsi ninavyohisi?’”

Kim anaweza kuamua kukazia fikira jinsi asivyotendewa kwa haki na jinsi mume wake anavyopuuza wajibu wake. Badala yake, anafanya jambo tofauti. Kim anasema: “Badala ya kuendelea kuudhika, nimejifunza kuwa ni afadhali kuchukua hatua ya kufanya amani. Mwishowe, sote wawili tunatulia na kuzungumzia mambo kwa amani.”—Yakobo 3:18.

4

LALAMIKO LA

“Mke wangu si mtiifu.”

KANUNI YA BIBLIA:

“Kichwa cha kila mwanamume ni Kristo.”1 WAKORINTHO 11:3.

Mume anayefikiri kuwa mke wake hajitiishi anapaswa kuchunguza kwanza kama yeye yuko tayari kujitiisha kwa Yesu Kristo, ambaye ndiye Kichwa chake. Anaweza kuonyesha ujitiisho wake kwa kufuata kielelezo cha Yesu.

Mtume Paulo aliandika: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Waefeso 5:25) Yesu ‘hakupiga ubwana juu’ ya wanafunzi wake. (Marko 10:42-44) Aliwapa wafuasi wake mwongozo ulio wazi na kuwarekebisha ilipohitajika. Lakini hakuwa mkali kamwe. Alikuwa mwenye huruma na alielewa kupungukiwa kwao. (Mathayo 11:29, 30; Marko 6:30, 31; 14:37, 38) Sikuzote alitanguliza mahitaji yao na si yake binafsi.—Mathayo 20:25-28.

Mume anahitaji kujiuliza swali hili: ‘Je, mtazamo wangu kuelekea ukichwa na wanawake kwa ujumla unaongozwa zaidi na mila kuliko mashauri na mifano katika Biblia?’ Kwa mfano, ungemwonaje mwanamke asiyekubaliana na maoni ya mume wake na kwa uthabiti lakini kwa heshima anaeleza maoni yake? Katika Biblia, Sara, mke wa Abrahamu anatajwa kuwa mke mwenye kujitiisha. (1 Petro 3:1, 6) Hata hivyo, alitoa maoni yake ilipohitajika, kama alivyofanya wakati ambapo Abrahamu alikosa kuona mambo fulani yaliyohatarisha familia yao.—Mwanzo 16:5; 21:9-12.

Ni wazi kuwa Abrahamu hakufanya Sara aogope kutoa maoni yake. Hakuwa dikteta. Vivyo hivyo, mume anayefuata mashauri ya Biblia hatamfanya mke wake aogope, akidai amfanyie lolote analotaka. Mke wake atamheshimu iwapo atatumia ukichwa wake kwa huruma.

Jinsi ambavyo wengine wametumia shauri hilo: James, ambaye anaishi Uingereza na ambaye alifunga ndoa miaka minane iliyopita, anasema: “Ninajifunza kutofanya maamuzi muhimu bila kushauriana na mke wangu. Ninajitahidi nisijifikirie mwenyewe tu. Badala yake, ninataka kutanguliza mahitaji yake.”

George anaishi Marekani na alifunga ndoa miaka 59 iliyopita. Anasema: “Nimejitahidi kumtendea mke wangu, si kama mtu duni, bali kama mwenzi mwenye akili na uwezo.”—Methali 31:10.

5

LALAMIKO LA

“Mume wangu haongozi mambo.”

KANUNI YA BIBLIA:

“Mwanamke mwenye hekima kwelikweli amejenga nyumba yake, lakini aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.”METHALI 14:1.

Ikiwa mume wako anasita kufanya maamuzi au kuongoza mambo nyumbani, unaweza kuchagua mojawapo ya mambo haya matatu: (1) Kumwonyesha kasoro zake kila wakati au (2) kunyakua daraka lake la ukichwa katika familia au (3) kumpongeza kutoka moyoni kwa jitihada zozote anazofanya. Ukichagua mambo mawili ya kwanza, utaibomoa nyumba yako kwa mikono yako mwenyewe. Lakini ukichagua jambo la tatu litakusaidia kujenga au kuimarisha ndoa yako.

Wanaume wengi wanathamini heshima kuliko upendo. Kwa hiyo, ukifanya mume wako ahisi anaheshimiwa—kwa kumfanya ahisi kuwa jitihada zake za kuiongoza familia zinafaa na zinathaminiwa—yaelekea atatimiza wajibu wake kwa njia bora zaidi. Bila shaka, mara kwa mara wewe na mume wako mtakosa kukubaliana kuhusu mambo fulani. Nyote wawili mnahitaji kuzungumzia mambo hayo. (Methali 18:13) Lakini maneno unayochagua na sauti unayotumia itachangia ama kubomoa au kujenga ndoa yako. (Methali 21:9; 27:15) Toa maoni yako kwa heshima, na yaelekea utapata matokeo unayotaka, yaani, mume asiyesita kuongoza familia yake.

Jinsi ambavyo wengine wametumia shauri hilo: Michele, anayeishi Marekani aliolewa miaka 30 iliyopita, naye anasema: “Kwa kuwa mama yangu alinilea mimi pamoja na dada zangu bila msaada wa mume, alikuwa mwanamke mwenye msimamo thabiti na mwenye kujitegemea. Nina mwelekeo wa kumwiga. Kwa hiyo, mimi hujitahidi daima kujitiisha ifaavyo. Kwa mfano, nimejifunza kuzungumza na mume wangu kabla sijafanya maamuzi.”

Rachel, anayeishi Australia na ambaye aliolewa miaka 21 iliyopita, aliathiriwa pia na malezi yake. Anasema: “Mama yangu hakuwa mtiifu kamwe kwa baba yangu. Walibishana siku zote na hakumheshimu. Nilipoolewa, niliiga tabia ya mama yangu mwanzoni. Lakini, baadaye nikajifunza kufuata shauri la Biblia kuhusu kuonyesha heshima. Sasa mimi na Mark tuna furaha zaidi katika ndoa yetu.”

6

LALAMIKO LA

“Siwezi kuendelea kuvumilia tabia zenye kuudhi za mwenzi wangu wa ndoa.”

KANUNI YA BIBLIA:

“Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.”WAKOLOSAI 3:13.

Mlipokuwa mkichumbiana, yaelekea ulikazia fikira sifa nzuri za mchumba wako na kupuuza kasoro zake. Je, unaweza kufanya hivyo leo? Bila shaka, unaweza kuwa na sababu nzuri ya kulalamika kuhusu tabia fulani ya mwenzi wako. Hata hivyo, jiulize, ‘Je, nitakazia fikira sifa gani za mwenzi wangu—zile mbaya au zile nzuri?’

Yesu alitumia mfano mzuri unaoonyesha uhitaji wa kutokazia fikira kasoro za wengine. Alisema: “Kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?” (Mathayo 7:3) Boriti ni nguzo iliyotumiwa kutegemeza paa la nyumba, nayo ni kubwa sana ikilinganishwa na unyasi. Yesu alimaanisha nini? “Kwanza toa boriti lililo katika jicho lako mwenyewe, na ndipo utakapoona waziwazi jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.”—Mathayo 7:5.

Kabla ya kutoa mfano huo, Yesu alikuwa ametoa onyo zito. Alisema: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa.” (Mathayo 7:1, 2) Ikiwa unataka Mungu akusamehe makosa yako—boriti lililo katika jicho lako—ni vema kwako kutozingatia kasoro za mwenzi wako.—Mathayo 6:14, 15.

Jinsi ambavyo wengine wametumia shauri hilo: Jenny, ambaye anaishi Uingereza aliolewa na Simon miaka tisa iliyopita, naye anasema: “Jambo linaloniudhi zaidi kumhusu mume wangu ni mwelekeo wake wa kutopanga mambo mapema, na hivyo kushughulikia mambo dakika ya mwisho. Sikutarajia hali iwe hivyo, kwa sababu tulipokuwa tukichumbiana, nilipendezwa na jinsi alivyoshughulikia mambo bila kusukumwa. Hata hivyo, mimi nimetambua kuwa nina kasoro pia, kama kujaribu kumwongoza katika kila jambo. Mimi na Simon tunajifunza kupuuza kasoro ndogondogo za kila mmoja wetu.”

Curt, mume wa Michele aliyenukuliwa awali, anasema: “Ukikazia fikiria tabia zenye kuudhi za mwenzi wako, kasoro hizo zitazidi kuwa kubwa. Mimi ninapendelea kukazia fikira sifa zilizofanya nimpende Michele.”

Siri ya Kufanikiwa

Mifano hiyo michache inaonyesha kuwa matatizo katika ndoa hayaepukiki, hata hivyo, yanaweza kutatuliwa. Ni nini siri ya kufanikiwa, au kufaulu? Sitawisha upendo kwa Mungu na utayari wa kufuata mashauri yaliyo katika Neno lake, Biblia.

Alex na Itohan, wanaoishi Nigeria walifunga ndoa zaidi ya miaka 20 iliyopita, na wamejua siri ya kufanikiwa katika ndoa. Alex anasema: “Nimetambua kuwa karibu kila tatizo katika ndoa linaweza kutatuliwa ikiwa mume na mke wanafuata kanuni za Biblia.” Mke wake anasema: “Tumetambua umuhimu wa kusali pamoja kwa ukawaida na kufuata mashauri ya Biblia ya kuwa wenye subira na kupendana kutoka moyoni. Sasa tuna matatizo machache ikilinganishwa na wakati tulipofunga ndoa.”

Je, ungependa kujifunza zaidi kuhusu jinsi mashauri yanayopatikana katika Neno la Mungu yanavyoweza kuisaidia familia yako? Ikiwa ndivyo, waombe Mashahidi wa Yehova wazungumzie pamoja nawe sura ya 14 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 63 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Je, tunatafuta wakati wa kuwa pamoja?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Je, mimi hujitahidi kutoa zaidi ya ninavyopokea?

[Picha katika ukurasa wa 6]

Je, ninachukua hatua ya kwanza ili kusuluhisha mabishano?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, mimi hufikiria maoni ya mke wangu kabla ya kufanya uamuzi?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, mimi hukazia fikira sifa nzuri za mwenzi wangu wa ndoa?