Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA NNE

Jinsi ya Kufanya Maisha ya Familia Yako Yawe Yenye Furaha

Jinsi ya Kufanya Maisha ya Familia Yako Yawe Yenye Furaha
  • Ni nini kinachohitajiwa ili kuwa mume mzuri?

  • Mwanamke anawezaje kufaulu kutimiza jukumu lake akiwa mke?

  • Ni nini kinachohitajiwa ili kuwa mzazi mzuri?

  • Watoto wanaweza kufanya nini ili maisha ya familia yawe yenye furaha?

1. Ni nini siri ya kuwa na familia yenye furaha?

YEHOVA MUNGU anataka familia yako iwe na maisha yenye furaha. Neno lake, Biblia, hutoa maagizo kwa kila mmoja katika familia na kuonyesha jukumu ambalo Mungu anataka kila mmoja atekeleze. Kila mmoja katika familia akitimiza jukumu lake kulingana na shauri la Mungu, familia itakuwa na furaha sana. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:28.

2. Furaha ya familia inategemea kutambua nini?

2 Furaha ya familia inategemea hasa kutambua kwamba familia ilianzishwa na Yehova, ambaye Yesu alimwita “Baba yetu.” (Mathayo 6:9) Baba yetu wa mbinguni ndiye aliyeanzisha kila familia duniani na bila shaka anajua kinacholeta furaha katika familia. (Waefeso 3:14, 15) Kwa hiyo, Biblia inafundisha nini kuhusu jukumu la kila mmoja katika familia?

FAMILIA ILIANZISHWA NA MUNGU

3. Biblia inaelezaje mwanzo wa familia ya wanadamu, na tunajuaje kwamba yale inayosema ni ya kweli?

3 Yehova aliwaumba wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, na kuwaunganisha kuwa mume na mke. Aliwaweka katika paradiso maridadi hapa duniani, bustani ya Edeni, na kuwaambia wazae watoto. Yehova alisema: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” (Mwanzo 1:26-28; 2:18, 21-24) Hii si hadithi au jambo la kukisiwa tu, kwa sababu Yesu alionyesha kwamba yale ambayo kitabu cha Mwanzo kinasema kuhusu mwanzo wa familia ni ya kweli. (Mathayo 19:4, 5) Ingawa tunapata matatizo mengi na maisha leo hayako kama Mungu alivyokusudia, hebu tuone ni kwa nini familia inaweza kuwa na furaha.

4. (a) Kila mmoja katika familia anawezaje kuchangia furaha ya familia? (b) Kwa nini familia itapata furaha ikijifunza kuhusu maisha ya Yesu?

4 Kila mmoja katika familia anaweza kuchangia furaha ya familia kwa kumwiga Mungu katika kuonyesha upendo. (Waefeso 5:1, 2) Hata hivyo, tunawezaje kumwiga Mungu na hatuwezi kumwona? Tunaweza kujifunza jinsi Yehova anavyotenda kwa sababu alimtuma Mwana wake mzaliwa wa kwanza kutoka mbinguni kuja duniani. (Yohana 1:14, 18) Alipokuwa duniani, Mwana huyo, Yesu Kristo, alimwiga sana Baba yake wa mbinguni hivi kwamba kumwona na kumsikiliza Yesu kulikuwa sawa na kuwa pamoja na Yehova na kumsikiliza. (Yohana 14:9) Kwa hiyo, kila mmoja wetu anaweza kuchangia zaidi furaha ya familia kwa kujifunza kuhusu upendo ambao Yesu alionyesha na kufuata mfano wake.

KIELELEZO KWA WAUME

5, 6. (a) Waume wanajifunza nini kutokana na jinsi Yesu anavyolitendea kutaniko? (b) Mtu anapaswa kufanya nini ili asamehewe dhambi zake?

5 Biblia inasema kwamba waume wanapaswa kuwatendea wake zao jinsi Yesu alivyowatendea wanafunzi wake. Fikiria mwongozo huu wa Biblia: “Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake . . . Vivyo hivyo, waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Yeye anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe, kwa maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo, kama vile Kristo pia anavyolitendea kutaniko.”Waefeso 5:23, 25-29.

6 Upendo wa Yesu kwa wanafunzi wake ni kielelezo bora kwa waume. Yesu ‘aliwapenda mpaka mwisho,’ akadhabihu uhai wake kwa ajili yao, hata ingawa hawakuwa wakamilifu. (Yohana 13:1; 15:13) Vivyo hivyo, waume wanahimizwa hivi: “Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) Ni nini kitakachomsaidia mume kufuata shauri hilo, hasa ikiwa nyakati nyingine mke wake hatendi kwa busara? Anapaswa kukumbuka makosa yake na anachopaswa kufanya ili kupata msamaha wa Mungu. Anapaswa kufanya nini? Anapaswa kumsamehe kila mtu anayemkosea, kutia ndani mke wake. Bila shaka, mke anapaswa kufanya vivyo hivyo. (Mathayo 6:12, 14, 15) Je, unaona ni kwa nini watu fulani husema kwamba ili ndoa zifanikiwe lazima wenzi wote wawili wawe tayari kusameheana?

7. Yesu alizingatia nini, naye aliwawekea waume kielelezo gani?

7 Waume wanapaswa kukumbuka pia kwamba sikuzote Yesu aliwajali wanafunzi wake. Alizingatia udhaifu wao na mahitaji yao ya kimwili. Kwa mfano, alisema hivi walipokuwa wamechoka: “Njooni, ninyi wenyewe, faraghani katika mahali pasipo na watu mpumzike kidogo.” (Marko 6:30-32) Wake pia wanastahili kuhangaikiwa kwa upendo. Biblia husema kwamba wao ni “chombo dhaifu zaidi” na waume wanaamriwa wawape “heshima.” Kwa nini? Kwa kuwa waume na wake pia wanashiriki “pendeleo lisilostahiliwa la uzima.” (1 Petro 3:7) Waume wanapaswa kukumbuka kwamba Mungu hupendezwa na uaminifu wa mtu wala si jinsia yake.—Zaburi 101:6.

8. (a) Mume ‘anayempenda mke wake, anajipendaje mwenyewe’? (b) Inamaanisha nini kwamba mume na mke ni “mwili mmoja”?

8 Biblia inasema kwamba mume “anayempenda mke wake anajipenda mwenyewe.” Hiyo ni kwa sababu mume na mke “si wawili tena, bali mwili mmoja,” kama Yesu alivyosema. (Mathayo 19:6) Hivyo basi, hawapaswi kufanya ngono na mtu mwingine yeyote. (Methali 5:15-21; Waebrania 13:4) Wataepuka kufanya hivyo ikiwa kila mmoja anajali mahitaji ya yule mwingine bila ubinafsi. (1 Wakorintho 7:3-5) Kikumbusho hiki pia kinafaa: “Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo.” Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama wanavyojipenda wenyewe, wakikumbuka kwamba watatoa hesabu kwa Yesu Kristo, aliye kichwa chao.—Waefeso 5:29; 1 Wakorintho 11:3.

9. Ni sifa gani ya Yesu inayotajwa katika Wafilipi 1:8, na kwa nini waume wanapaswa kuwaonyesha wake zao sifa hiyo?

9 Mtume Paulo alizungumzia ‘upendo mwororo alio nao Kristo Yesu.’ (Wafilipi 1:8) Wororo wa Yesu ulikuwa sifa yenye kuburudisha, iliyowavutia wanawake ambao walikuwa wanafunzi wake. (Yohana 20:1, 11-13, 16) Nao wake hutamani sana waume zao wawapende kwa wororo.

KIELELEZO KWA WAKE

10. Yesu anawawekeaje wake mfano?

10 Familia ni kama shirika, na ili lifanye kazi vizuri, linahitaji kuwa na kichwa. Hata Yesu anajitiisha kwa Yule aliye Kichwa chake. “Kichwa cha Kristo ni Mungu” kama vile “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Wakorintho 11:3) Kujitiisha kwa Yesu chini ya ukichwa wa Mungu ni mfano mzuri kwa kuwa sote tuna kichwa ambaye tunapaswa kujitiisha kwake.

11. Mke anapaswa kumwonaje mume wake, na mwenendo wake unaweza kuwa na matokeo gani?

11 Wanaume wasio wakamilifu hufanya makosa na mara nyingi wao hupungukiwa katika jukumu lao la kuwa vichwa vya familia. Kwa hiyo, mke anapaswa kufanya nini? Hapaswi kudharau mambo ambayo mume wake anafanya au kujaribu kumnyang’anya ukichwa. Mke anapaswa kukumbuka kwamba roho ya utulivu na upole ina thamani kubwa machoni pa Mungu. (1 Petro 3:4) Akiwa na roho hiyo, itakuwa rahisi kwake kuonyesha utii wa kimungu hata katika hali ngumu. Isitoshe, Biblia inasema: “Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Lakini vipi akikataa kujitiisha chini ya Kristo akiwa Kichwa chake? Biblia inawasihi wake hivi: “Jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”1 Petro 3:1, 2.

12. Kwa nini si kosa mke kueleza maoni yake kwa heshima?

12 Mume awe ni mwamini au la, mke hatakuwa akimvunjia heshima ikiwa ataeleza maoni yake kwa njia ya busara hata kama yanatofautiana na ya mume. Huenda maoni yake yakawa sawa, na yanaweza kufaidi familia nzima ikiwa mume atamsikiliza. Ingawa Abrahamu hakukubaliana na mke wake Sara alipopendekeza jinsi ya kutatua tatizo fulani la familia, Mungu alimwambia: “Sikiliza sauti yake.” (Mwanzo 21:9-12) Bila shaka, mume anapofanya uamuzi ambao haupingani na sheria ya Mungu, mke wake anapaswa kuonyesha anajitiisha kwake kwa kuunga mkono uamuzi huo.—Matendo 5:29; Waefeso 5:24.

Sara aliwawekea wake mfano gani mzuri?

13. (a) Andiko la Tito 2:4, 5 linawasihi wanawake ambao wameolewa wafanye nini? (b) Biblia inasema nini kuhusu kutengana na kutalikiana?

13 Mke anaweza kutimiza jukumu lake kwa kutunza familia. Kwa mfano, Biblia inaonyesha kwamba wanawake ambao wameolewa wanapaswa ‘kuwapenda waume zao, kuwapenda watoto wao, kuwa na utimamu wa akili, safi kiadili, wafanyakazi nyumbani, wema, wakijitiisha kwa waume zao wenyewe.’ (Tito 2:4, 5) Mke ambaye pia ni mama anayefanya hivyo, atapendwa na kuheshimiwa daima na familia yake. (Methali 31:10, 28) Lakini kwa kuwa ndoa ni muungano wa watu wasio wakamilifu, huenda hali fulani wasizoweza kuvumilia zikawafanya watengane au kutalikiana. Biblia inaruhusu kutengana hali fulani zinapotokea. Hata hivyo, kutengana hakupaswi kuchukuliwa kivivi hivi tu, kwa kuwa Biblia inashauri: “Mke hapaswi kuondoka kwa mume wake; . . . na mume hapaswi kumwacha mke wake.” (1 Wakorintho 7:10, 11) Msingi pekee wa Kimaandiko wa talaka ni uasherati.—Mathayo 19:9.

MFANO BORA KWA WAZAZI

14. Yesu aliwatendeaje watoto, nao watoto wanahitaji nini kutoka kwa wazazi wao?

14 Yesu aliwawekea wazazi mfano bora wa jinsi ya kuwatendea watoto. Wengine walipojaribu kuwazuia watoto wadogo wasimkaribie, Yesu alisema hivi: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.” Kisha Biblia inasema kwamba ‘aliwachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.’ (Marko 10:13-16) Kwa kuwa Yesu alitumia wakati pamoja na watoto, je, hupaswi kufanya hivyo na watoto wako? Wanahitaji wakati wako mwingi. Unahitaji kutumia wakati kuwafundisha kwani Yehova anawaagiza wazazi wafanye hivyo.—Kumbukumbu la Torati 6:4-9.

15. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwalinda watoto wao?

15 Kadiri ulimwengu huu unavyozidi kuwa mbovu, ndivyo watoto wanavyohitaji wazazi watakaowalinda dhidi ya watu wanaotaka kuwaumiza, kama wale wanaowatendea vibaya watoto kingono. Fikiria jinsi Yesu alivyowalinda wanafunzi wake ambao aliwapenda sana na kuwaita “watoto wadogo.” Alipokamatwa ili auawe baadaye, Yesu alifanya mipango ili wanafunzi wake watoroke. (Yohana 13:33; 18:7-9) Ukiwa mzazi, unapaswa kuwa macho kuona njia ambazo Ibilisi anatumia kujaribu kuwaumiza watoto wako. Unahitaji kuwaonya mapema. * (1 Petro 5:8) Huu ndio wakati ambapo hali yao ya kimwili, ya kiroho, na ya kiadili imo hatarini zaidi kuliko wakati mwingine wowote.

Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea watoto?

16. Wazazi wanaweza kujifunza nini kutokana na njia ambayo Yesu alishughulikia kutokamilika kwa wanafunzi wake?

16 Usiku uliotangulia kifo cha Yesu, wanafunzi wake walibishana kuhusu ni nani aliye mkubwa kati yao. Kwa kuwa Yesu aliwapenda, badala ya kuwakasirikia, aliendelea kuwasihi kwa maneno na kuwawekea mfano. (Luka 22:24-27; Yohana 13:3-8) Ikiwa wewe ni mzazi, je, unaona jinsi unavyoweza kufuata mfano wa Yesu unapowarekebisha watoto wako? Ni kweli kwamba wanahitaji nidhamu, lakini inapaswa kutolewa kwa “kiwango kinachofaa” wala si kwa hasira. Hupaswi kuzungumza nao bila kufikiri “kama kwa upanga unaochoma.” (Yeremia 30:11; Methali 12:18) Nidhamu inapaswa kutolewa kwa njia ambayo mtoto ataithamini baadaye.—Waefeso 6:4; Waebrania 12:9-11.

MFANO KWA WATOTO

17. Yesu aliwawekea watoto mfano bora katika njia zipi?

17 Je, watoto wanaweza kujifunza kutoka kwa Yesu? Ndiyo, wanaweza! Kupitia mfano wake, Yesu alionyesha jinsi watoto wanavyopaswa kuwatii wazazi wao. Alisema: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema.” Akaongezea: “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yohana 8:28, 29) Yesu alimtii Baba yake wa mbinguni, na Biblia inawaambia watoto wawatii wazazi wao. (Waefeso 6:1-3) Ingawa Yesu alikuwa mtoto mkamilifu, aliwatii wazazi wake, Yusufu na Maria, ambao hawakuwa wakamilifu. Hapana shaka kwamba hilo lilichangia furaha ya kila mmoja katika familia ya Yesu!—Luka 2:4, 5, 51, 52.

18. Kwa nini Yesu alimtii Baba yake wa mbinguni sikuzote, na watoto humfurahisha nani wanapowatii wazazi wao leo?

18 Je, watoto wanaweza kutambua njia wanazoweza kumwiga Yesu zaidi na kuwafurahisha wazazi wao? Ni kweli kwamba nyakati nyingine watoto huona ni vigumu kuwatii wazazi wao, hata hivyo, Mungu anataka watoto watii. (Methali 1:8; 6:20) Yesu alimtii Baba yake wa mbinguni sikuzote, hata hali zilipokuwa ngumu. Pindi moja, Mungu alipomtaka Yesu afanye jambo gumu sana, Yesu alisema: “Niondolee kikombe hiki [au takwa fulani].” Hata hivyo, Yesu alifanya mapenzi ya Mungu kwa sababu alitambua kwamba Baba yake anajua mwendo bora wa kufuata. (Luka 22:42) Kwa kujifunza kutii, watoto watawafurahisha wazazi wao na Baba yao wa mbinguni. *Methali 23:22-25.

Vijana wanapaswa kuzingatia nini wanaposhawishiwa?

19. (a) Shetani huwashawishi watoto jinsi gani? (b) Mwenendo mbaya wa watoto unaweza kuwaathirije wazazi?

19 Ibilisi alimshawishi Yesu, na tunaweza kuwa na hakika kwamba atawashawishi watoto pia wafanye mambo mabaya. (Mathayo 4:1-10) Shetani Ibilisi hutumia mikazo ya marafiki ambayo inaweza kuwa mikali sana. Basi ni muhimu sana watoto wasishirikiane na wale wanaotenda mabaya. (1 Wakorintho 15:33) Dina, binti ya Yakobo alishirikiana na watu ambao hawakuwa wakimwabudu Yehova, na kufanya hivyo kulimletea matatizo makubwa. (Mwanzo 34:1, 2) Hebu wazia jinsi familia inavyoweza kuumia mmoja wao akihusika katika mwenendo mpotovu kingono!—Methali 17:21, 25.

SIRI YA KUWA NA FAMILIA YENYE FURAHA

20. Ili kuwa na maisha ya familia yenye furaha, kila mmoja katika familia anapaswa kufanya nini?

20 Shauri la Biblia linapotumiwa, inakuwa rahisi kukabiliana na matatizo katika familia. Kutumia shauri hilo ndiyo siri ya kuwa na familia yenye furaha. Kwa hiyo waume, wapendeni wake zenu na kuwatendea kama Yesu anavyolitendea kutaniko lake. Wake, tiini ukichwa wa waume zenu na mfuate mfano wa mke mwenye uwezo anayetajwa katika Methali 31:10-31. Wazazi, wazoezeni watoto wenu. (Methali 22:6) Akina baba, ‘simamieni nyumba zenu kwa njia nzuri.’ (1 Timotheo 3:4, 5; 5:8) Nanyi watoto, watiini wazazi wenu. (Wakolosai 3:20) Hakuna yeyote katika familia aliye mkamilifu kwa kuwa wote hufanya makosa. Kwa hiyo, nyenyekeeni na kuombana msamaha.

21. Tuna tarajio gani zuri, na tunawezaje kuwa na maisha ya familia yenye furaha sasa?

21 Kwa kweli, Biblia ina mashauri na maagizo mengi yenye faida kuhusu maisha ya familia. Isitoshe, Biblia hutufundisha kuhusu ulimwengu mpya wa Mungu na paradiso ya kidunia itakayojaa watu wenye furaha wanaomwabudu Yehova. (Ufunuo 21:3, 4) Hilo ni tarajio zuri kama nini! Hata sasa, tunaweza kuwa na maisha ya familia yenye furaha kwa kufuata maagizo ya Mungu yaliyo katika Neno lake, Biblia.

^ fu. 15 Habari kuhusu jinsi ya kuwalinda watoto zinapatikana katika sura ya 32 ya kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Mtoto ana haki ya kutotii ikiwa mzazi anamwomba avunje sheria ya Mungu.—Matendo 5:29.