Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sura ya Kumi na Nane

Ubatizo na Uhusiano Wako Pamoja na Mungu

Ubatizo na Uhusiano Wako Pamoja na Mungu
  • Ubatizo wa Kikristo hufanywaje?

  • Unapaswa kuchukua hatua zipi ili ustahili kubatizwa?

  • Mtu hujiwekaje wakfu kwa Mungu?

  • Ni sababu gani ya pekee inayomfanya mtu abatizwe?

1. Kwa nini ofisa Mwethiopia wa makao ya kifalme alitaka kubatizwa?

“TAZAMA! Maji; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?” Swali hilo liliulizwa katika karne ya kwanza na ofisa Mwethiopia wa makao ya kifalme. Mkristo aliyeitwa Filipo, alikuwa amemthibitishia kwamba Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa. Akiwa amechochewa na yale aliyokuwa amejifunza katika Maandiko, Mwethiopia huyo alichukua hatua. Alionyesha kwamba anataka kubatizwa!—Matendo 8:26-36.

2. Kwa nini unapaswa kufikiria kwa uzito kuhusu ubatizo?

2 Ikiwa umejifunza kwa makini sura za kwanza za kitabu hiki na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, huenda ukauliza, ‘Ni nini kinachonizuia nisibatizwe?’ Kufikia sasa umejifunza kuhusu ahadi ya Biblia ya uzima wa milele katika Paradiso. (Luka 23:43; Ufunuo 21:3, 4) Pia umejifunza ukweli kuhusu hali ya wafu na tumaini la ufufuo. (Mhubiri 9:5; Yohana 5:28, 29) Huenda umekuwa ukihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova na umejionea upendo walio nao ambao hutambulisha ibada ya kweli. (Yohana 13:35) Zaidi ya yote, huenda umeanza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu.

3. (a) Yesu aliwapa wafuasi wake amri gani? (b) Ubatizo wa maji hufanywaje?

3 Unawezaje kuonyesha kwamba unataka kumtumikia Mungu? Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza.” (Mathayo 28:19) Yesu mwenyewe alituwekea kielelezo alipobatizwa katika maji. Hakunyunyiziwa wala kumwagiliwa maji kidogo kichwani. (Mathayo 3:16) Neno “batiza” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “zamisha.” Kwa hiyo, ubatizo wa Kikristo unamaanisha kuzamisha, au kutumbukiza kabisa ndani ya maji.

4. Ubatizo wa maji huonyesha nini?

4 Kila mtu anayetaka kuwa na uhusiano pamoja na Yehova Mungu anapaswa kubatizwa katika maji. Ubatizo huonyesha waziwazi kwamba unataka kumtumikia Mungu. Pia unaonyesha kwamba unatamani kufanya mapenzi ya Yehova. (Zaburi 40:7, 8) Hata hivyo, ili ustahili kubatizwa, ni lazima uchukue hatua fulani.

UNAHITAJI IMANI NA UJUZI

5. (a) Kabla ya kubatizwa, mtu anapaswa kuchukua hatua gani kwanza? (b) Kwa nini mikutano ya Kikristo ni muhimu?

5 Tayari umeanza kuchukua hatua ya kwanza. Jinsi gani? Labda kwa kujifunza Biblia hatua kwa hatua na kuendelea kupata ujuzi kumhusu Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Yohana 17:3) Hata hivyo, kuna mengi ya kujifunza. Wakristo wanataka ‘wajazwe ujuzi sahihi wa mapenzi yake [Mungu].’ (Wakolosai 1:9) Kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kutakusaidia kufanya hivyo. Ni muhimu kuhudhuria mikutano hiyo. (Waebrania 10:24, 25) Kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kutakusaidia kuongeza ujuzi juu ya Mungu.

Kupata ujuzi sahihi kuhusu Neno la Mungu ni hatua muhimu ambayo mtu anapaswa kuchukua ili astahili kubatizwa

6. Mtu anapaswa kuwa na ujuzi wa Biblia kiasi gani ili astahili kubatizwa?

6 Ni kweli kwamba si lazima ujue kila jambo katika Biblia ndipo ustahili kubatizwa. Yule ofisa Mwethiopia wa makao ya kifalme alikuwa na kiasi fulani cha ujuzi, hata hivyo, alihitaji kusaidiwa ili kuelewa sehemu fulani za Maandiko. (Matendo 8:30, 31) Vivyo hivyo, wewe pia unahitaji kujifunza mengi zaidi. Kwa kweli, hutafikia mwisho wa kujifunza kumhusu Mungu. (Mhubiri 3:11) Hata hivyo, kabla ya kubatizwa, unahitaji kujua na kukubali mafundisho ya msingi ya Biblia. (Waebrania 5:12) Mafundisho hayo yanatia ndani kweli kuhusu hali ya wafu na umuhimu wa jina la Mungu na Ufalme wake.

7. Kujifunza Biblia kunapaswa kuwa na matokeo gani kwako?

7 Ujuzi peke yake hautoshi kwa maana “bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza [Mungu] vema.” (Waebrania 11:6) Biblia inatuambia kwamba watu fulani wa jiji la kale la Korintho waliposikia ujumbe wa Kikristo ‘walianza kuamini na kubatizwa.’ (Matendo 18:8) Vivyo hivyo, kadiri unavyozidi kujifunza Biblia, ndivyo unavyopaswa kuwa na imani zaidi kwamba hiyo ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Kujifunza Biblia kunapaswa kukusaidia kuwa na imani katika ahadi za Mungu, na kuamini kwamba dhabihu ya Yesu inaweza kukuokoa.—Yoshua 23:14; Matendo 4:12; 2 Timotheo 3:16, 17.

KUZUNGUMZA NA WENGINE KUHUSU KWELI ZA BIBLIA

8. Ni nini kitakachokuchochea kuzungumza na wengine mambo ambayo umejifunza?

8 Kadiri unavyozidi kuwa na imani, ndivyo utakavyoona ikiwa rahisi kuzungumza na wengine mambo ambayo umejifunza. (Yeremia 20:9) Utachochewa sana kuzungumza na wengine kuhusu Mungu na makusudi yake.—2 Wakorintho 4:13.

Imani inapaswa kukuchochea uzungumze na wengine kuhusu mambo ambayo umejifunza

9, 10. (a) Unaweza kuanza kuwahubiria nani kweli ya Biblia? (b) Unapaswa kufanya nini ikiwa unataka kushiriki katika kazi ya kuhubiri pamoja na Mashahidi wa Yehova?

9 Unaweza kuanza kuzungumza na wengine kuhusu kweli za Biblia kwa kuanzisha mazungumzo kwa busara pamoja na watu wa ukoo, marafiki, majirani, na wafanyakazi wenzako. Baada ya muda, huenda ukataka kuhubiri rasmi pamoja na Mashahidi wa Yehova. Ukifikia hatua hiyo, mjulishe Shahidi anayekufundisha Biblia. Ikiwa unastahili kuwa mhubiri, mipango itafanywa ili wewe na mwalimu wako mwe na mazungumzo pamoja na wazee wawili wa kutaniko.

10 Kufanya hivyo kutakuwezesha kuwafahamu wazee Wakristo wanaolichunga kundi la Mungu. (Matendo 20:28; 1 Petro 5:2, 3) Wazee hao wakiona kwamba unaelewa na kuamini mafundisho ya msingi ya Biblia, unaishi kupatana na kanuni za Mungu na kwa kweli unataka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, watakujulisha kwamba unastahili kushiriki katika huduma ukiwa mhubiri ambaye hajabatizwa wa habari njema.

11. Huenda watu fulani wakahitaji kufanya marekebisho gani ili wastahili kuwa wahubiri?

11 Kwa upande mwingine, huenda ukahitaji kurekebisha maisha na mazoea yako ili ustahili kuwa mhubiri. Hilo linaweza kutia ndani kuacha mazoea fulani mabaya. Kwa hiyo, kabla ya kuomba kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, unahitaji kuacha kabisa dhambi nzito kama vile ukosefu wa adili katika ngono, ulevi, na kutumia dawa za kulevya.—1 Wakorintho 6:9, 10; Wagalatia 5:19-21.

KUTUBU NA KUGEUKA

12. Kwa nini mtu anapaswa kutubu?

12 Kuna hatua nyingine zinazotangulia ubatizo. Mtume Petro alisema: “Tubuni na mgeuke ili dhambi zenu zipate kufutwa.” (Matendo 3:19) Kutubu ni kusikitika kikweli kwa sababu ya jambo ulilofanya. Mtu anapaswa kutubu ikiwa aliishi maisha yasiyo ya adili na hata yule ambaye amekuwa akiishi maisha safi kiadili anapaswa kufanya hivyo pia. Kwa nini? Kwa sababu wanadamu wote ni watenda dhambi na wanahitaji msamaha wa Mungu. (Waroma 3:23; 5:12) Kabla ya kujifunza Biblia, hukujua mapenzi ya Mungu. Kwa hiyo hungeweza kuishi kulingana na mapenzi yake. Basi, unapaswa kutubu.

13. Kugeuka kunamaanisha nini?

13 Baada ya kutubu, lazima ‘ugeuke.’ Haitoshi tu kusikitika. Unahitaji kukataa maisha yako ya zamani na kuazimia kabisa kufanya yaliyo mema kuanzia sasa na kuendelea. Ni lazima utubu na kugeuka kabla ya kubatizwa.

KUJIWEKA WAKFU

14. Kabla ya kubatizwa, unahitaji kuchukua hatua gani muhimu?

14 Kuna hatua nyingine muhimu inayopaswa kuchukuliwa kabla ya ubatizo. Ni lazima ujiweke wakfu kwa Yehova Mungu.

Je, umejiweka wakfu kwa Mungu katika sala?

15, 16. Kujiweka wakfu kwa Mungu kunamaanisha nini, na ni nini humchochea mtu kufanya hivyo?

15 Unapojiweka wakfu kwa Yehova Mungu katika sala inayotoka moyoni, unamwahidi kwamba umejitoa kwake peke yake kwa umilele wote. (Kumbukumbu la Torati 6:15) Hata hivyo, kwa nini ujitoe kwake? Tuseme kwamba mwanamume ameanza kumchumbia mwanamke. Kadiri anavyozidi kuona sifa zake nzuri ndivyo anavyozidi kuvutiwa naye. Kwa kawaida, baada ya muda atamwomba wafunge ndoa. Ni kweli kwamba kufunga ndoa kutamwongezea majukumu. Hata hivyo, upendo utamchochea kuchukua hatua hiyo muhimu.

16 Baada ya kumjua na kumpenda Yehova, utachochewa kumtumikia bila kusita wala masharti yoyote kuhusiana na ibada. Yeyote anayetaka kumfuata Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, lazima “ajikane mwenyewe.” (Marko 8:34) Tunajikana wenyewe kwa kuhakikisha kwamba mapendezi na miradi yetu binafsi haituzuii kumtii Mungu kikamili. Basi, kabla ya kubatizwa, ni lazima jambo kuu maishani mwako liwe kufanya mapenzi ya Yehova Mungu.—1 Petro 4:2.

KUTOOGOPA KUSHINDWA

17. Kwa nini huenda watu fulani wakasita kujiweka wakfu kwa Mungu?

17 Watu fulani husita kujiweka wakfu kwa Yehova kwa sababu wanaogopa kuchukua hatua hiyo muhimu. Huenda wakaogopa kuwajibika mbele za Mungu wakiwa Wakristo waliojiweka wakfu. Kwa kuwa wanaogopa kumkosea na kumkasirisha Yehova, wanaona ni afadhali wasijiweke wakfu kwake.

18. Ni nini kinachoweza kukuchochea ujiweke wakfu kwa Yehova?

18 Unapoendelea kujifunza kumpenda Yehova, utachochewa kujiweka wakfu kwake na kujitahidi kuishi kulingana na wakfu huo. (Mhubiri 5:4) Baada ya kujiweka wakfu, bila shaka utajitahidi ‘kutembea kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye.’ (Wakolosai 1:10) Kwa sababu unampenda Mungu, haitakuwa vigumu kwako kufanya mapenzi yake. Bila shaka utakubaliana na mtume Yohana, aliyeandika: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 Yohana 5:3.

19. Kwa nini hupaswi kuogopa kujiweka wakfu kwa Yehova?

19 Haimaanishi kwamba unahitaji kuwa mkamilifu ili ujiweke wakfu kwa Mungu. Yehova anajua uwezo wako naye hatarajii kamwe ufanye mambo usiyoweza. (Zaburi 103:14) Anataka ufanikiwe naye atakutegemeza na kukusaidia. (Isaya 41:10) Bila shaka, ukimtumaini Yehova kabisa, “atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

KUONYESHA WAKFU KWA KUBATIZWA

20. Kwa nini mtu anapaswa kuonyesha hadharani kwamba amejiweka wakfu kwa Yehova?

20 Kufikiria kwa uzito mambo ambayo tumezungumzia kwaweza kukusaidia kuamua kujiweka wakfu kwa Yehova katika sala. Kila mtu anayempenda Mungu kikweli lazima pia ‘afanye tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.’ (Waroma 10:10) Mtu hufanyaje tangazo hilo?

Ubatizo humaanisha kufa, au kuacha maisha ya zamani, na kuanza maisha mapya ya kufanya mapenzi ya Mungu

21, 22. Unawezaje kutoa “tangazo la hadharani” la imani yako?

21 Mjulishe mwangalizi-msimamizi wa kutaniko lenu kwamba ungependa kubatizwa. Atapanga wazee fulani wapitie nawe maswali kadhaa yanayohusu mafundisho ya msingi ya Biblia. Wazee hao wakiona kwamba unastahili, watakujulisha kwamba utabatizwa katika kusanyiko linalofuata. * Kwa kawaida hotuba inayoeleza maana ya ubatizo hutolewa katika makusanyiko hayo. Kisha msemaji huwaomba wote watakaobatizwa wajibu maswali mawili rahisi ikiwa njia moja ya kutoa “tangazo la hadharani” la imani yao.

22 Ubatizo ndio unaoonyesha hadharani kwamba umejiweka wakfu kwa Mungu na sasa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wanaobatizwa huzamishwa kabisa majini ili kuonyesha hadharani kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova.

MAANA YA UBATIZO WAKO

23. Inamaanisha nini kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu”?

23 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wangebatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mathayo 28:19) Hilo linamaanisha kwamba anayetaka kubatizwa anatambua mamlaka ya Yehova Mungu na Yesu Kristo. (Zaburi 83:18; Mathayo 28:18) Pia anatambua kazi na utendaji wa roho takatifu au nguvu ya utendaji ya Mungu.—Wagalatia 5:22, 23; 2 Petro 1:21.

24, 25. (a) Ubatizo huonyesha nini? (b) Ni swali gani linalohitaji kujibiwa?

24 Hata hivyo, ubatizo si kutumbukizwa majini tu. Unawakilisha jambo fulani muhimu sana. Kuzamishwa majini huonyesha kwamba umekufa, au umeacha maisha yako ya zamani. Na kuibuka kutoka majini huonyesha kwamba sasa umeanza maisha mapya ya kufanya mapenzi ya Mungu. Kumbuka pia kwamba umejiweka wakfu kwa Yehova Mungu mwenyewe wala si kwa kazi fulani, mradi fulani, mtu fulani, au tengenezo fulani. Kujiweka wakfu na kubatizwa ni mwanzo wa kuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu.—Zaburi 25:14.

25 Ubatizo haukuhakikishii wokovu. Mtume Paulo aliandika: “Endeleeni kuufanyia kazi wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.” (Wafilipi 2:12) Ubatizo ni mwanzo tu. Kwa hiyo basi, Unawezaje kukaa katika upendo wa Mungu? Sura ya mwisho ya kitabu hiki itajibu swali hilo.

^ fu. 21 Ubatizo hufanywa kwa ukawaida katika makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova ya kila mwaka.