Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA TATU

Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?

Mungu Ana Kusudi Gani kwa Dunia?
  • Mungu ana kusudi gani kwa wanadamu?

  • Mungu amepingwaje?

  • Maisha yatakuwaje duniani wakati ujao?

1. Ni nini kusudi la Mungu kwa dunia?

KUSUDI la Mungu kwa dunia ni zuri ajabu. Yehova anataka dunia ijae watu wenye furaha na afya. Biblia inasema kwamba ‘Mungu alipanda bustani katika Edeni na kuchipusha kila mti wenye kutamanika kwa macho ya mtu na ulio mwema kwa chakula.’ Baada ya Mungu kumuumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, aliwaweka katika makao hayo mazuri na kuwaambia: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwanzo 1:28; 2:8, 9, 15) Kwa hiyo Mungu alikusudia wanadamu wawe na watoto, waieneze bustani hiyo duniani pote, na kuwatunza wanyama.

2. (a) Tunajuaje kwamba kusudi la Mungu kwa dunia litatimia? (b) Biblia inasema nini kuhusu wanadamu kuishi milele?

2 Je, unafikiri kusudi la Yehova Mungu kwamba wanadamu waishi katika dunia iliyo paradiso litatimia? Mungu anasema hivi: “Mimi nimesema hilo; pia nitalitimiza.” (Isaya 46:9-11; 55:11) Naam, Mungu atatimiza kusudi lake! Kuhusu dunia, anasema kwamba “hakuiumba tu bila sababu,” bali “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Mungu alitaka dunia ikaliwe na watu wa aina gani? Naye alitaka wakae humo kwa muda gani? Biblia inajibu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

3. Ni hali gani zenye kuhuzunisha zilizopo duniani leo, na ni maswali gani yanayozuka?

3 Ni wazi kwamba kusudi la Mungu halijatimia bado. Leo watu wanakuwa wagonjwa na kufa; hata wanapigana na kuuana. Mambo yaliharibika. Hata hivyo, hapana shaka kwamba Mungu hakukusudia dunia iwe kama ilivyo leo! Ni nini kilichotukia? Kwa nini kusudi la Mungu halijatimia? Hakuna kitabu chochote cha kihistoria kilichoandikwa na mwanadamu kinaweza kutuambia kwa sababu matatizo yalianzia mbinguni.

ADUI ATOKEA

4, 5. (a) Ni nani hasa aliyetumia nyoka kuzungumza na Hawa? (b) Mtu aliyekuwa mzuri na mnyoofu anawezaje kugeuka na kuwa mwizi?

4 Kitabu cha kwanza cha Biblia kinataja kuhusu mpinzani wa Mungu aliyetokea katika bustani ya Edeni. Anaitwa “nyoka,” ingawa hakuwa mnyama halisi. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia anaitwa “Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” Pia anaitwa “yule nyoka wa zamani.” (Mwanzo 3:1; Ufunuo 12:9) Malaika huyo mwenye nguvu, au kiumbe asiyeonekana mwenye mwili wa kiroho, alitumia nyoka kuzungumza na Hawa, kama vile mtu mwenye ustadi anavyoweza kufanya ionekane kana kwamba sauti inatoka katika mwanasesere au sanamu. Bila shaka kiumbe huyo alikuwapo Mungu alipokuwa akiitayarisha dunia kwa ajili ya wanadamu.—Ayubu 38:4, 7.

5 Kwa kuwa uumbaji wote wa Yehova ni mkamilifu, basi, ni nani aliyemfanya “Shetani Ibilisi”? Kwa ufupi, mmoja kati ya wana wenye nguvu wa Mungu aligeuka akawa Ibilisi. Jinsi gani? Leo mtu ambaye wakati fulani alikuwa mzuri na mnyoofu anaweza kugeuka na kuwa mwizi. Hilo linawezekanaje? Huenda mtu akaruhusu tamaa mbaya iingie moyoni mwake. Akiendelea kuisitawisha, tamaa hiyo inaweza kuwa na nguvu sana. Kisha akipata nafasi, anaweza kutenda kulingana na tamaa hiyo mbaya ambayo imekuwa ikisitawi moyoni mwake.—Yakobo 1:13-15.

6. Mmoja kati ya wana wenye nguvu wa Mungu aligeukaje na kuwa Shetani Ibilisi?

6 Ndivyo ilivyokuwa kuhusu Shetani Ibilisi. Huenda alimsikia Mungu akiwaambia Adamu na Hawa wazae watoto na kuijaza dunia. (Mwanzo 1:27, 28) Haikosi Shetani aliwaza hivi: ‘Kwani, si wanadamu hao wote wanaweza kuniabudu mimi badala ya kumwabudu Mungu!’ Kwa hiyo, tamaa mbaya ikaanza kusitawi moyoni mwake. Mwishowe, akaamua kumdanganya Hawa kwa kumwambia uwongo kumhusu Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Basi, akawa “Ibilisi,” jina linalomaanisha “Mchongezi.” Wakati huohuo akawa “Shetani,” jina linalomaanisha “Mpinzani.”

7. (a) Kwa nini Adamu na Hawa walikufa? (b) Kwa nini wazao wote wa Adamu huzeeka na kufa?

7 Kwa kutumia uwongo na ujanja, Shetani Ibilisi aliwafanya Adamu na Hawa wamwasi Mungu. (Mwanzo 2:17; 3:6) Mwishowe, wakafa kwa sababu ya uasi kama Mungu alivyokuwa amesema. (Mwanzo 3:17-19) Kwa kuwa Adamu alipoteza ukamilifu alipoasi, wazao wake wote walirithi dhambi kutoka kwake. (Waroma 5:12) Hali hiyo inaweza kulinganishwa na sufuria inayotumiwa kuoka mikate. Ikiwa sufuria hiyo imejikunja, kila mkate utakaookwa katika sufuria hiyo utakuwaje? Kila mkate utakuwa na alama, au kasoro. Vivyo hivyo, kila mwanadamu amerithi “kasoro” ya kutokamilika kutoka kwa Adamu. Ndiyo sababu wanadamu wote huzeeka na kufa.—Waroma 3:23.

8, 9. (a) Yaelekea Shetani alidai nini? (b) Kwa nini Mungu hakuwaharibu waasi hao mara moja?

8 Shetani alipowashawishi Adamu na Hawa wafanye dhambi dhidi ya Mungu, alianzisha uasi. Alikuwa akipinga utawala wa Yehova. Ni kana kwamba Shetani alikuwa akisema: ‘Mungu ni mtawala mbaya. Yeye husema uwongo na kuwanyima raia wake vitu vizuri. Wanadamu hawahitaji kutawaliwa na Mungu. Wanaweza kujiamulia yaliyo mema na mabaya. Na watakuwa na maisha mazuri zaidi nikiwatawala.’ Mungu angeshughulikiaje upinzani huo? Watu fulani husema kwamba afadhali Mungu angewaua tu waasi hao. Lakini je, kufanya hivyo kungetatua upinzani wa Shetani? Je, kungethibitisha kwamba utawala wa Mungu ndio unaofaa?

9 Yehova hangewaua waasi hao mara moja kwa sababu yeye ni Mungu mwenye haki kabisa. Aliamua kwamba wakati ulihitajiwa ili kutatua upinzani wa Shetani kwa njia yenye kuridhisha na kuthibitisha kwamba Ibilisi ni mwongo. Kwa hiyo Mungu akaamua kwamba atawaacha wanadamu wajitawale kwa muda fulani chini ya uvutano wa Shetani. Sura ya 11 ya kitabu hiki itaeleza sababu iliyomfanya Yehova aamue hivyo na kuruhusu muda wa kutosha upite kabla ya kutatua masuala hayo. Hata hivyo, kwa sasa ni vizuri kujiuliza hivi: Je, Adamu na Hawa walikuwa na sababu ya kumwamini Shetani ambaye hakuwa amewafanyia jambo lolote zuri? Je, walikuwa na msingi wowote wa kuamini kwamba Yehova ambaye alikuwa amewapa vyote walivyokuwa navyo, ni mwongo na mkatili? Wewe ungefanyaje?

10. Unawezaje kuunga mkono upande wa Yehova na kumpinga Shetani?

10 Ni vizuri kufikiria maswali hayo kwa sababu kila mmoja wetu anakabili masuala hayo leo. Naam, wewe una nafasi ya kuunga mkono upande wa Yehova na kumpinga Shetani. Unaweza kumkubali Yehova kuwa Mtawala na kuonyesha kwamba Shetani ni mwongo. (Zaburi 73:28; Methali 27:11) Inasikitisha kwamba, kati ya mabilioni ya watu ulimwenguni pote, ni wachache tu wanaoamua kufanya hivyo. Hilo linatokeza swali muhimu, Je, kweli Biblia inafundisha kwamba Shetani anatawala ulimwengu huu?

NI NANI ANAYEUTAWALA ULIMWENGU HUU?

Shetani angewezaje kumwahidi Yesu falme zote za ulimwengu ikiwa hazikuwa zake?

11, 12. (a) Kushawishiwa kwa Yesu kunaonyeshaje kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu? (b) Ni nini kingine kinachothibitisha kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu?

11 Yesu hakuwa na shaka yoyote kwamba Shetani ndiye mtawala wa ulimwengu huu. Pindi moja Shetani alimwonyesha Yesu kimuujiza “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” Kisha Shetani akamwahidi Yesu: “Nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” (Mathayo 4:8, 9; Luka 4:5, 6) Hebu fikiria: Je, Shetani angeweza kumshawishi Yesu kwa kutoa ahadi hiyo ikiwa hakuwa mtawala wa falme hizo? Yesu hakupinga kwamba serikali zote hizo za ulimwengu hazikuwa za Shetani. Bila shaka, Yesu angepinga ikiwa hazikuwa za Shetani.

12 Bila shaka, Yehova ndiye Mungu Mweza-Yote, Muumba wa ulimwengu wetu wa ajabu. (Ufunuo 4:11) Hata hivyo, Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova Mungu au Yesu Kristo ni watawala wa ulimwengu huu. Yesu alimwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31; 14:30; 16:11) Hata Biblia inamwita Shetani Ibilisi “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (2 Wakorintho 4:3, 4) Kuhusu mpinzani huyo au Shetani, mtume Mkristo Yohana aliandika: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”—1 Yohana 5:19.

JINSI ULIMWENGU WA SHETANI UTAKAVYOONDOLEWA

13. Kwa nini tunahitaji ulimwengu mpya?

13 Ulimwengu unazidi kuwa hatari mwaka baada ya mwaka. Kuna majeshi mengi yanayopigana, wanasiasa wafisadi, viongozi wa kidini wanafiki, na wahalifu sugu. Haiwezekani kuubadili ulimwengu kwa ujumla. Biblia inasema kwamba hivi karibuni Mungu atauondolea mbali ulimwengu huu mbovu katika vita vya Har–Magedoni. Kisha ataleta ulimwengu mpya wenye uadilifu.—Ufunuo 16:14-16.

14. Mungu amemchagua nani awe Mtawala katika Ufalme Wake, na hilo lilitabiriwaje?

14 Yehova Mungu alimchagua Yesu Kristo awe Mtawala wa Ufalme au serikali Yake ya mbinguni. Biblia ilitabiri hivi zamani: “Kwa maana kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu, kuna mwana ambaye tumepewa; na utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake. Naye ataitwa . . . Mkuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.” (Isaya 9:6, 7) Kuhusu serikali hiyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Kama tutakavyoona baadaye katika kitabu hiki, karibuni Ufalme wa Mungu utaondolea mbali serikali zote za ulimwengu huu nao utatawala badala ya serikali hizo. (Danieli 2:44) Kisha Ufalme wa Mungu utaleta paradiso duniani.

ULIMWENGU MPYA U KARIBU!

15. “Dunia mpya” ni nini?

15 Biblia inatuhakikishia hivi: “Kulingana na ahadi yake [Mungu] tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13; Isaya 65:17) Nyakati nyingine Biblia inapotaja “dunia,” inamaanisha watu wanaoishi duniani. (Mwanzo 11:1) Kwa hiyo “dunia mpya” yenye uadilifu ni jamii ya watu watakaopata kibali cha Mungu.

16. Ni zawadi gani yenye thamani sana ambayo Mungu atawapa wale walio na kibali chake, na tunapaswa kufanya nini ili tuipokee?

16 Yesu aliahidi kwamba katika ulimwengu mpya unaokuja, wale wanaopata kibali cha Mungu watapokea zawadi ya “uzima wa milele.” (Marko 10:30) Tafadhali fungua Yohana 3:16 na Yohana 17:3 katika Biblia yako, na usome yale ambayo Yesu alisema tunapaswa kufanya ili tupate uzima wa milele. Sasa ona baraka zinazotajwa katika Biblia zitakazofurahiwa na wale wanaostahili kupokea zawadi hiyo ya pekee kutoka kwa Mungu katika dunia itakayokuwa Paradiso.

17, 18. Tunawezaje kuwa na hakika kwamba kutakuwa na amani na usalama duniani pote?

17 Hakutakuwa na uovu, vita, uhalifu, na ujeuri. “Mtu mwovu hatakuwako tena . . . Bali wapole wataimiliki dunia.” (Zaburi 37:10, 11) Kutakuwa na amani kwa sababu ‘Mungu atakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9; Isaya 2:4) Kisha “mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena”—yaani, milele!—Zaburi 72:7.

18 Waabudu wa Yehova wataishi kwa usalama. Nyakati zote Waisraeli katika nyakati za Biblia walipomtii Mungu, waliishi kwa usalama. (Mambo ya Walawi 25:18, 19) Litakuwa jambo zuri ajabu kufurahia usalama kama huo katika Paradiso!—Isaya 32:18; Mika 4:4.

19. Tunajuaje kwamba kutakuwa na chakula kingi katika ulimwengu mpya wa Mungu?

19 Hakutakuwa na upungufu wa chakula. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Yehova Mungu atawabariki waadilifu wake, na “hakika dunia itatoa mazao yake.”—Zaburi 67:6.

20. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba dunia nzima itakuwa paradiso?

20 Dunia nzima itakuwa paradiso. Kutakuwa na makao na bustani zenye kupendeza katika sehemu zilizokuwa zimeharibiwa na wanadamu wenye dhambi. (Isaya 65:21-24; Ufunuo 11:18) Kadiri wakati unavyopita, sehemu za dunia zinazokaliwa zitapanuka mpaka dunia yote iwe yenye kupendeza na kuzaa sana kama bustani ya Edeni. Na Mungu hatakosa kamwe ‘kufumbua mkono wake na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’—Zaburi 145:16.

21. Ni nini kinachoonyesha kwamba kutakuwa na amani kati ya wanadamu na wanyama?

21 Kutakuwa na amani kati ya wanadamu na wanyama. Wanyama mwitu na wa kufugwa watalisha pamoja. Hata mtoto mdogo hataogopa wanyama ambao ni hatari leo.—Isaya 11:6-9; 65:25.

22. Ni hatua gani itakayochukuliwa kuhusiana na magonjwa?

22 Magonjwa hayatakuwapo. Akiwa Mtawala wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu, Yesu ataponya watu kwa kiwango kikubwa zaidi kuliko alivyofanya alipokuwa duniani. (Mathayo 9:35; Marko 1:40-42; Yohana 5:5-9) Hatimaye, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24; 35:5, 6.

23. Kwa nini ufufuo utaleta shangwe mioyoni mwetu?

23 Wapendwa waliokufa watafufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele. Wote wanaolala katika kifo walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa. “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29.

24. Unaonaje kuhusu kuishi katika Paradiso duniani?

24 Wale wanaoamua kujifunza kuhusu Muumba wetu Mtukufu, Yehova Mungu na kumtumikia wana tumaini zuri kama nini! Yesu alikuwa akizungumzia Paradiso ya wakati ujao hapa duniani alipomwahidi hivi yule mtenda maovu aliyetundikwa pamoja naye: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Tunapaswa kujifunza mengi zaidi kumhusu Yesu Kristo, atakayetumiwa kuleta baraka hizo zote.