Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA PILI

Biblia—Kitabu Kutoka kwa Mungu

Biblia—Kitabu Kutoka kwa Mungu
  • Biblia inatofautianaje na vitabu vingine?

  • Biblia inawezaje kukusaidia kukabiliana na matatizo yako?

  • Kwa nini unaweza kuamini unabii mbalimbali ulio katika Biblia?

1, 2. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Biblia ni zawadi nzuri kutoka kwa Mungu?

HEBU wazia jinsi ulivyohisi ulipopata zawadi ya pekee kutoka kwa rafiki yako. Haikosi ulisisimuka na kufurahi kwelikweli. Mtu anapokupa zawadi anaonyesha kwamba anakuthamini. Bila shaka, ulimshukuru rafiki yako kwa sababu ya zawadi hiyo.

2 Biblia ni zawadi kutoka kwa Mungu, nasi tunapaswa kuithamini kwelikweli. Kitabu hicho cha pekee hufunua mambo ambayo hatungejua kwa njia nyingine yoyote. Kwa mfano, Biblia hutuambia kuhusu kuumbwa kwa mbingu zenye nyota, dunia, hali kadhalika mwanamume na mwanamke wa kwanza. Biblia ina kanuni zenye kutegemeka zinazotusaidia kukabiliana na matatizo na mahangaiko ya maisha. Inaeleza jinsi Mungu atakavyotimiza kusudi lake na kuleta hali bora duniani. Biblia ni zawadi nzuri kama nini!

3. Yehova anaonyesha nini kwa kutupa Biblia, na kwa nini hilo linatuchangamsha?

3 Pia, Biblia ni zawadi inayochangamsha moyo kwa sababu inatueleza jambo fulani kumhusu Mpaji mwenyewe, Yehova Mungu. Kwa kuwa ametupa Biblia, ni wazi kwamba anataka tumjue vizuri. Kwa kweli, Biblia inaweza kukusaidia kumkaribia Yehova.

4. Ni nini kinachokupendeza kuhusu kugawanywa kwa Biblia?

4 Leo, watu wengi wana Biblia. Biblia imechapishwa katika lugha zaidi ya 2,300 ikiwa nzima au kwa sehemu na kwa hiyo zaidi ya asilimia 90 ya watu ulimwenguni wanaweza kuipata. Kwa wastani, Biblia zaidi ya milioni moja hugawanywa kila juma! Mabilioni ya nakala za Biblia zimechapishwa zikiwa nzima au kwa sehemu. Kwa kweli, hakuna kitabu kingine kilicho kama Biblia.

“Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya” inapatikana katika lugha nyingi

5. Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu’ jinsi gani?

5 Isitoshe, Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu.’ (2 Timotheo 3:16) Jinsi gani? Biblia yenyewe inajibu hivi: “Wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Kwa mfano: Huenda babu akamwomba mjukuu wake amwandikie barua. Mjukuu huyo ataandika mawazo na maagizo ya babu huyo. Kwa hiyo, kwa kweli barua hiyo ni ya babu huyo wala si ya mjukuu wake. Vivyo hivyo, Biblia ina ujumbe wa Mungu wala si wa watu waliotumiwa kuiandika. Kwa hiyo, Biblia kwa kweli ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.

NI SAHIHI NA YENYE UPATANO

6, 7. Kwa nini upatano wa Biblia ni wa pekee sana?

6 Biblia iliandikwa kwa kipindi cha zaidi ya miaka 1,600. Walioiandika walikuwa watu wa hali mbalimbali walioishi nyakati tofauti. Baadhi yao walikuwa wakulima, wavuvi, na wachungaji. Wengine walikuwa manabii, waamuzi, na wafalme. Luka aliyeandika Injili alikuwa daktari. Licha ya malezi mbalimbali ya watu walioiandika, Biblia ina upatano tangu mwanzo mpaka mwisho. *

7 Kitabu cha kwanza cha Biblia kinatuambia jinsi matatizo ya wanadamu yalivyoanza. Kitabu cha mwisho kinaonyesha kwamba dunia yote itakuwa paradiso, au bustani. Biblia nzima inazungumzia mambo ambayo yametukia kwa maelfu ya miaka, na kila sehemu inatusaidia kuelewa jinsi kusudi la Mungu linavyotimizwa. Upatano wa Biblia hauna kifani, na hilo halishangazi kwa kuwa Biblia ni kitabu kutoka kwa Mungu.

8. Toa mifano inayoonyesha kwamba Biblia ni sahihi kisayansi.

8 Biblia ni sahihi kisayansi. Hata ilizungumzia mambo yaliyokuja kugunduliwa baadaye. Kwa mfano, kitabu cha Mambo ya Walawi kina sheria walizopewa Waisraeli wa zamani kuhusu usafi na kuwatenga wagonjwa ili kuepuka maambukizo ingawa mataifa jirani hayakujua mambo hayo. Wakati ambapo watu walikuwa na maoni yasiyo sahihi kuhusu umbo la dunia, Biblia ilisema kwamba dunia ni mviringo au duara. (Isaya 40:22) Biblia ilisema kwa usahihi kwamba dunia ‘imetundikwa pasipo na kitu.’ (Ayubu 26:7) Biblia si kitabu cha sayansi. Hata hivyo, inapozungumzia mambo ya sayansi, hufanya hivyo kwa usahihi. Tunatarajia kitabu kutoka kwa Mungu kiwe hivyo, sivyo?

9. (a) Biblia ni sahihi na inategemeka kihistoria jinsi gani? (b) Unajifunza nini kuhusu Biblia kutokana na unyoofu wa watu walioiandika?

9 Pia, Biblia ni sahihi na inategemeka kuhusu mambo ya kihistoria. Inasimulia mambo hususa yaliyotokea. Mbali na kutaja majina ya watu, inaonyesha pia ukoo wao. * Tofauti na wanahistoria wa ulimwengu ambao mara nyingi hawataji kushindwa kwa mataifa yao, waandikaji wa Biblia walikuwa wanyoofu, hata waliandika kuhusu makosa yao wenyewe na ya taifa lao. Kwa mfano, katika kitabu cha Biblia cha Hesabu, mwandikaji Musa anakiri kosa lake kubwa lililofanya aadhibiwe vikali. (Hesabu 20:2-12) Si rahisi kuona unyoofu wa aina hiyo katika masimulizi mengine ya kihistoria lakini unapatikana katika Biblia kwa sababu ni kitabu cha Mungu.

KITABU CHENYE HEKIMA

10. Kwa nini haishangazi kwamba Biblia ni kitabu chenye faida?

10 Biblia ‘ni yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo,’ kwa sababu imeongozwa na roho ya Mungu. (2 Timotheo 3:16) Naam, Biblia ni kitabu chenye faida. Inaeleza kinaganaga hali ya wanadamu. Hilo halishangazi kwa kuwa Mtungaji wake ni Yehova Mungu, Muumba! Anaelewa fikira na hisia zetu kuliko tunavyozielewa. Isitoshe, Yehova anajua tunachohitaji ili tuwe na furaha. Anajua pia mambo tunayopaswa kuepuka.

11, 12. (a) Yesu alizungumzia mambo gani katika Mahubiri yake ya Mlimani? (b) Ni mambo gani mengine muhimu yanayozungumziwa katika Biblia, na kwa nini shauri lake lina faida sikuzote?

11 Fikiria yale yanayoitwa Mahubiri ya Mlimani ya Yesu katika Mathayo sura ya 5 mpaka ya 7. Katika mahubiri hayo bora, Yesu alizungumzia mambo mbalimbali kama vile jinsi ya kupata furaha ya kweli, jinsi ya kutatua mizozano, jinsi ya kusali, na jinsi ya kuwa na maoni yanayofaa kuelekea vitu vya kimwili. Maneno ya Yesu yanachochea na yana faida leo kama yalivyokuwa alipoyasema.

12 Kanuni fulani za Biblia zinahusu maisha ya familia, mazoea ya kazi, na mahusiano pamoja na wengine. Kanuni za Biblia zinawahusu watu wote, na shauri lake ni lenye faida sikuzote. Kupitia nabii Isaya, Mungu anataja hekima iliyo katika Biblia: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.”—Isaya 48:17.

KITABU CHA UNABII

Isaya, mwandikaji wa Biblia alitabiri kuanguka kwa Babiloni

13. Yehova alimwongoza nabii Isaya aandike habari gani hususa kuhusu Babiloni?

13 Biblia ina unabii mwingi, baadhi yake umetimizwa. Kwa mfano, kupitia nabii Isaya aliyeishi katika karne ya nane K.W.K., Yehova alitabiri kwamba jiji la Babiloni lingeharibiwa. * (Isaya 13:19; 14:22, 23) Habari hususa zilitolewa kuonyesha jinsi ambavyo uharibifu huo ungetokea. Majeshi yanayovamia yangekausha mto wa Babiloni na kuingia jijini bila hata kupigana. Si hayo tu. Unabii wa Isaya hata ulitaja jina la mfalme ambaye angeshinda Babiloni, yaani, Koreshi.—Isaya 44:27–45:2.

14, 15. Unabii wa Isaya kuhusu Babiloni ulitimizwaje?

14 Miaka 200 hivi baadaye, usiku wa Oktoba 5/6, 539 K.W.K., jeshi lilipiga kambi karibu na Babiloni. Ni nani aliyekuwa amiri wa jeshi hilo? Mfalme wa Uajemi anayeitwa Koreshi. Kwa hiyo, wakati ulikuwa umefika wa kutimizwa kwa unabii huo wa ajabu. Lakini je, jeshi la Koreshi lingevamia Babiloni bila kupigana kama ilivyotabiriwa?

15 Wababiloni walikuwa na sherehe usiku huo na walihisi wakiwa salama katika jiji hilo lenye kuta kubwa. Wakati huohuo, Koreshi alikuwa akigeuza kwa ustadi mkondo wa maji ya mto uliokuwa ukipita katika jiji hilo. Muda si muda maji yalikuwa yamepungua kiasi cha kwamba majeshi yake yangeweza kuvuka mto na kukaribia kuta za jiji. Hata hivyo, jeshi la Koreshi lingeingiaje Babiloni lenye kuta kubwa? Kwa sababu moja au nyingine, usiku huo malango ya jiji hilo hayakuwa yamefungwa!

16. (a) Isaya alitabiri nini kuhusu mambo ambayo yangepata jiji la Babiloni? (b) Unabii wa Isaya kuhusu ukiwa wa Babiloni ulitimizwaje?

16 Ilitabiriwa hivi kuhusu Babiloni: “Hatakaliwa kamwe, wala hatakuwa na makao kwa kizazi baada ya kizazi. Na hapo Mwarabu hatapiga hema lake, na hakuna wachungaji watakaoruhusu makundi yao kulala hapo.” (Isaya 13:20) Unabii huo ulitabiri hata mambo ambayo yangetokea baada ya jiji hilo kuanguka. Ulionyesha kwamba jiji la Babiloni lingeachwa ukiwa daima. Unaweza kuona utimizo wa maneno hayo. Eneo lenye ukiwa la Babiloni la kale, kilometa 80 hivi kusini mwa Baghdad, nchini Iraq, linathibitisha kwamba unabii huu wa Yehova kupitia nabii Isaya umetimizwa: “Nami nitamfagia kwa ufagio wa maangamizi.”—Isaya 14:22, 23. *

Magofu ya Babiloni

17. Kutimizwa kwa unabii wa Biblia kunaimarishaje imani?

17 Kuchunguza jinsi Biblia ilivyo kitabu chenye unabii wa kutegemeka ni jambo lenye kuimarisha imani, sivyo? Ikiwa Yehova tayari ametimiza ahadi zake za wakati uliopita, tuna kila sababu ya kuamini kwamba atatimiza pia ahadi yake ya kuifanya dunia iwe paradiso. (Hesabu 23:19) Kwa kweli tuna “tumaini la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.”—Tito 1:2. *

“NENO LA MUNGU LIKO HAI”

18. Mtume Mkristo Paulo anasema maneno gani yenye kuchochea kuhusu “neno la Mungu”?

18 Kutokana na mambo ambayo tumechunguza katika sura hii, ni wazi kwamba kwa kweli Biblia ni kitabu cha pekee. Hata hivyo, thamani yake haitokani tu na upatano wake, usahihi wake wa kisayansi na wa kihistoria, hekima iliyomo, na unabii uliomo unaotegemeka. Mtume Mkristo Paulo aliandika: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.”—Waebrania 4:12.

19, 20. (a) Biblia inawezaje kukusaidia ujichunguze? (b) Unawezaje kuonyesha kwamba unaithamini Biblia ikiwa zawadi ya pekee kutoka kwa Mungu?

19 Kusoma “neno” la Mungu au ujumbe ulio katika Biblia kunaweza kubadili maisha yetu. Kunaweza kutusaidia tujichunguze vizuri zaidi. Huenda tukadai kwamba tunampenda Mungu, lakini jinsi tunavyoitikia mafundisho ya Neno lake, Biblia, lililoongozwa na roho kutaonyesha wazi mawazo yetu na hata mwelekeo wa moyo wetu.

20 Kwa kweli, Biblia ni kitabu kutoka kwa Mungu. Ni kitabu ambacho tunapaswa kusoma, kujifunza, na kukipenda. Onyesha kwamba unaithamini zawadi hiyo kutoka kwa Mungu kwa kuendelea kujifunza yaliyomo. Kwa kufanya hivyo, utaelewa hata zaidi kusudi la Mungu kwa wanadamu. Sura inayofuata itazungumzia kusudi hilo na jinsi litakavyotimizwa.

^ fu. 6 Ijapokuwa watu fulani husema kwamba sehemu fulani za Biblia zinapingana, madai hayo hayana msingi. Ona sura ya 7 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 9 Kwa mfano, angalia ukoo wa Yesu unaofafanuliwa katika Luka 3:23-38.

^ fu. 13 Ufupisho K.W.K. humaanisha “Kabla ya Wakati wa Kawaida,” ambao ni sahihi zaidi kuliko K.K. (“Kabla ya Kristo”). Ufupisho W.K. humaanisha “Wakati wa Kawaida,” ambao mara nyingi huitwa A.D., au Anno Domini, ikimaanisha “Katika Mwaka wa Bwana Wetu.”

^ fu. 16 Unaweza kupata habari zaidi kuhusu unabii wa Biblia, katika broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, ukurasa wa 27-29, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 17 Kuharibiwa kwa Babiloni ni mfano mmoja tu wa unabii wa Biblia ambao umetimizwa. Mifano mingine inatia ndani kuharibiwa kwa Tiro na Ninawi. (Ezekieli 26:1-5; Sefania 2:13-15) Pia, unabii wa Danieli ulitabiri milki za ulimwengu ambazo zingetawala baada ya Babiloni. Zilitia ndani Ugiriki na muungano wa Umedi na Uajemi. (Danieli 8:5-7, 20-22) Unaweza kupata habari zaidi kuhusu unabii mbalimbali unaomhusu Masihi uliotimizwa na Yesu Kristo katika nyongeza “Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa.”