Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Msikiaji wa Sala Anaruhusu Watu Wateseke?

Kwa Nini Msikiaji wa Sala Anaruhusu Watu Wateseke?

Kwa Nini Msikiaji wa Sala Anaruhusu Watu Wateseke?

HATA ingawa watu fulani husali, bado wanashuku ikiwa kuna Mungu. Kwa nini wanatilia shaka? Labda ni kwa sababu wanaona watu wakiteseka sana ulimwenguni. Je, umewahi kujiuliza kwa nini Mungu ameruhusu watu wateseke?

Je, kweli Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa katika hali waliyo nayo sasa, yaani, hali ya kutokamilika na kupatwa na mateso? Ingekuwa vigumu kumheshimu mungu ambaye angewaumba wanadamu ili wateseke. Lakini fikiria mfano huu: Ikiwa ungetazama gari jipya huku ukivutiwa nalo, kisha utambue kwamba limeharibika upande mmoja, je, ungefikiria kwamba lilitengenezwa hivyo? Bila shaka, la! Huenda ungefikia mkataa kwamba lilitengenezwa “bila kasoro” na kwamba liliharibiwa na mtu au kitu fulani.

Vivyo hivyo, ikiwa tungetazama na kuvutiwa na mpangilio na ubuni wa ajabu katika mazingira yetu kisha tuone machafuko na ufisadi unaowasumbua wanadamu, tungefikia mkataa gani? Biblia inafundisha kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wa kwanza wakiwa wakamilifu lakini baadaye wakajisababishia matatizo. (Kumbukumbu la Torati 32:​4, 5) Habari njema ni kwamba Mungu ameahidi kuondoa matatizo hayo kwa kuwarudishia wanadamu watiifu hali yao ya ukamilifu. Hata hivyo, kwa nini amekawia?

Kwa Nini Amekawia Sana?

Jibu linahusiana na swali lililozuka kuhusu ni nani anayepaswa kuwatawala wanadamu. Yehova hakukusudia kamwe wanadamu wajitawale wenyewe. Angekuwa Mtawala wao. Biblia yenyewe inasema: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wanadamu wa kwanza waliamua kuasi utawala wa Mungu. Kwa kumwasi Mungu, wakawa watenda dhambi. (1 Yohana 3:4) Matokeo ni kuwa walipoteza hali yao ya ukamilifu na wakajisababishia matatizo wao wenyewe na wazao wao pia.

Kwa maelfu ya miaka, Yehova amewaruhusu wanadamu wajitawale, na historia imethibitisha kwamba wanadamu hawana uwezo wa kujitawala wenyewe. Imeonyesha kwamba serikali zote za wanadamu zinasababisha mateso. Hakuna hata moja ambayo imefaulu kuondoa vita, uhalifu, ukosefu wa haki, au magonjwa.

Mungu Atarekebishaje Mambo?

Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni Mungu ataleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Petro 3:13) Wale tu wanaoamua kuwapenda wenzao na kumpenda Mungu ndio watakaoruhusiwa kuishi katika ulimwengu huo.​—Kumbukumbu la Torati 30:15, 16, 19, 20.

Pia, Biblia inasema kwamba katika “siku ya hukumu” ambayo inakaribia haraka, Mungu ataondoa mateso na wale wanaoyasababisha. (2 Petro 3:7) Baadaye, Yesu Kristo, Mtawala aliyechaguliwa na Mungu, atawatawala wanadamu watiifu. (Danieli 7:13, 14) Utawala wa Yesu utatimiza mambo gani? Biblia inasema: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”​—Zaburi 37:11.

Akiwa Mfalme mbinguni, Yesu ataondoa matatizo kama vile magonjwa, kuzeeka, na kifo ambayo yalianza baada ya wanadamu kumwasi Mungu ambaye ni “chemchemi ya uzima.” (Zaburi 36:9) Yesu atawaponya watu wote wanaojitiisha chini ya utawala wake wenye upendo. Chini ya utawala wake, ahadi hizi za Biblia zitatimizwa:

▪ “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’ Watu wanaokaa katika nchi hiyo watakuwa wamesamehewa kosa lao.”​—Isaya 33:24.

▪ “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”​—Ufunuo 21:4.

Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba hivi karibuni Mungu ataondoa mateso yote? Kwa sasa, hatupaswi kuwa na shaka kwamba anasikiliza sala zetu, hata kama ameruhusu wanadamu wateseke kwa muda.

Mungu yupo. Anaweza kukusikiliza, hata unapomweleza kuhusu mambo yanayokutia uchungu na huzuni. Na anatamani kuona wakati ambapo utafurahia maisha bila kuwa na shaka na bila maumivu yoyote.