Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Mungu

Mungu Anaposamehe, je, Yeye Husahau?

Mungu Anaposamehe, je, Yeye Husahau?

JIBU la swali hilo ni, ndiyo. Kuhusiana na wale ambao anawaonyesha kibali Yehova anaahidi hivi: “Nitalisamehe kosa lao, na dhambi yao sitaikumbuka tena.” (Yeremia 31:34) Kwa hiyo, Yehova anatuhakikishia kwamba anapowasamehe wakosaji wanaotubu, haendelei kuyakumbuka makosa yao. Hata hivyo, je, inamaanisha kwamba Muumba wa ulimwengu wote ulio mkubwa sana hawezi kukumbuka dhambi ambazo tayari amesamehe? Maneno ya Ezekieli yanatusaidia kuelewa jinsi Mungu anavyosamehe na kusahau.​Soma  Ezekieli 18:​19-22.

Akimtumia nabii Ezekieli kama msemaji wake, Yehova alitangaza hukumu dhidi ya wakaaji wasio waaminifu wa Yuda na Yerusalemu. Kwa ujumla, taifa lote lilikuwa limeacha ibada ya Yehova na nchi ilikuwa imejaa jeuri. Yehova alitabiri kwamba Jiji la Yerusalemu lingeharibiwa na Wababiloni. Lakini hata alipokuwa akitangaza hukumu, Yehova alitoa ujumbe wa tumaini. Kila mtu alikuwa na hiari ya kuchagua, na angewajibika kwa uamuzi ambao angefanya.​—Mistari ya 19, 20.

Vipi ikiwa mtu angeacha kufanya mambo mabaya na kuanza kufanya mema? Yehova alisema hivi: “Kwa habari ya mwovu, ikiwa atageuka na kuziacha dhambi zake zote ambazo ametenda naye hakika ashike sheria zangu na kutenda haki na uadilifu, hakika yeye ataendelea kuishi. Hatakufa.” (Mstari wa 21) Ndiyo, Yehova alikuwa “tayari kusamehe” mtenda-dhambi aliyegeuka na kuacha mabaya, na hivyo kuonyesha toba ya kweli.​—Zaburi 86:5.

Vipi kuhusu dhambi alizokuwa ametenda? “Makosa yake yote ambayo ametenda​—hayo hayatakumbukwa juu yake,” Yehova akaeleza. (Mstari wa 22) Ona kwamba makosa ya mtenda dhambi anayetubu “hayatakumbukwa juu yake.” Kwa nini hilo ni jambo muhimu?

Katika Biblia neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kumbuka” linaweza kumaanisha mengi zaidi ya kukumbuka wakati uliopita. Kuhusiana na neno hilo, kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Mara nyingi, kwa kweli, [li]namaanisha kuchukua hatua au linatumiwa pamoja na kitenzi.” Kwa hiyo, “kukumbuka” kunaweza kumaanisha “kuchukua hatua.” Hivyo basi, Yehova anaposema kwamba dhambi za mtenda-dhambi anayetubu ‘hazitakumbukwa juu yake,’ Anamaanisha kwamba hatamchukulia hatua mtu huyo kwa sababu ya dhambi alizotubu. *

Maneno ya andiko la Ezekieli 18:21, 22 yanaonyesha vizuri jinsi Mungu anavyosamehe kwa njia inayotugusa moyo. Yehova anapotusamehe dhambi zetu, hatatuchukulia hatua kamwe wakati ujao kwa kutegemea dhambi hizo. Badala yake, anazitupa dhambi za wanaotubu nyuma yake. (Isaya 38:17) Ni kana kwamba anafuta kumbukumbu ya dhambi hizo.​—Matendo 3:19.

Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, tunahitaji rehema za Mungu. Zaidi ya yote, sisi hutenda dhambi mara nyingi. (Waroma 3:23) Lakini Yehova anataka tufahamu kwamba tukitubu kikweli, yeye yuko tayari kutusamehe. Na anapotusamehe, anasahau, yaani, hatakumbuka tena dhambi zetu ili atuhukumu au kutuadhibu tena. Jambo hili linatufariji kama nini! Je, rehema za Mungu hazikuchochei utake kumkaribia hata zaidi?

Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa kwa Mwezi wa Julai:

Ezekieli 6-20

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Vivyo hivyo, “kukumbuka dhambi” kunaweza kumaanisha “kuchukua hatua dhidi ya waovu.”​—Yeremia 14:10.