Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutoka Katika Neno La Mungu

Viumbe wa Roho Wanahusikaje Katika Maisha Yetu?

Viumbe wa Roho Wanahusikaje Katika Maisha Yetu?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Malaika ni nani?

Malaika ni viumbe wa roho wanaoishi mbinguni. Wana uhai wa hali ya juu kuliko wanadamu. Mungu wa kweli, ambaye yeye mwenyewe ni roho, aliwaumba malaika kabla hajaumba dunia. (Ayubu 38:4, 7; Mathayo 18:10) Yehova amezungukwa na mamilioni ya malaika waaminifu.​—Soma Zaburi 103:20, 21; Danieli 7:9, 10.

2. Je malaika wanawasaidia watu?

Malaika walimsaidia mwanamume mwaminifu aliyeitwa Loti. Aliishi kwenye jiji ambalo Mungu alikusudia kuliangamiza kwa sababu ya uovu wa watu wa jiji hilo. Malaika wawili walimwambia Loti na familia yake wakimbie. Watu wengine waliona onyo hilo kuwa mzaha na wakalipuuza. Lakini Loti na binti zake waliokoka kwa sababu walitii onyo ambalo Mungu alitoa kupitia malaika hao.​—Soma Mwanzo 19:1, 13-17, 26.

Kulingana na Biblia, malaika wanawasaidia watu leo kwa kuongoza kazi ya wale wanaohubiri kwa uaminifu habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Habari hizo njema zinatia ndani maonyo. Kama ilivyokuwa katika siku za Loti, maonyo yanayotolewa leo si mzaha. Yanatoka kwa Mungu kupitia malaika.​—Soma Ufunuo 1:1; 14:6, 7.

Mungu anaweza kutumia malaika kutuimarisha tunapokabiliana na majaribu. Alitumia malaika kumwimarisha Yesu.​—Soma Luka 22:41-43.

Hivi karibuni, Mungu atawatumia malaika kwa njia nyingine, yaani, kuangamiza watu waovu wanaosababisha kuteseka. Jambo hilo litawaletea wanadamu kitulizo.​—Soma 2 Wathesalonike 1:6-8.

3. Roho waovu wanawaathirije wanadamu?

Kama vile ambavyo wanadamu wengi hapa duniani wameamua kumwasi Mungu, vilevile huko mbinguni malaika wengi wamemwasi Mungu. (2 Petro 2:4) Malaika hao waasi wanaitwa roho waovu. Kiongozi wao ni Shetani, Ibilisi. Shetani na malaika zake waovu wanapotosha wanadamu.​—Soma Ufunuo 12:9.

Shetani ametumia biashara zenye ufisadi, serikali za wanadamu, na dini za uwongo ili kuwashawishi watu na kuwageuza wamwache Mungu. Kwa hiyo, Shetani ndiye anayesababisha ukosefu wa haki, machafuko, na mateso yanayowapata wanadamu.​—Soma 1 Yohana 5:19.

4. Roho waovu wanawapotoshaje wanadamu?

Shetani amewadanganya watu wengi kwa kuwafanya waamini kwamba watu waliokufa wanageuka na kuwa roho wanaoweza kuwasiliana nao. Kinyume na hilo, Biblia inasema kwamba watu waliokufa hawawezi kufanya jambo lolote. (Mhubiri 9:5) Lakini, mara nyingi roho waovu huwadanganya watu kwa kuiga sauti za wapendwa waliokufa. (Isaya 8:19) Roho waovu huwapotosha wengine kupitia mazoea ya kuwasiliana na pepo, kutafuta ishara za bahati, uaguzi na unajimu. Neno la Mungu linatuonya tuepuke mazoea hayo. Kwa hiyo, tunapaswa kuharibu chochote kinachohusiana na roho waovu au uchawi.​—Soma Kumbukumbu la Torati 18:10, 11; Matendo 19:19.

Ikiwa tunampenda Yehova hatupaswi kuogopa roho waovu. Tunapojifunza Neno la Mungu na kutenda kulingana na yale tunayojifunza, tunampinga Ibilisi na kumkaribia Mungu. Yehova ana nguvu nyingi kuliko roho waovu. Malaika zake waaminifu wanaweza kutuimarisha tunapokabili hali ngumu.​—Soma Zaburi 34:7; Yakobo 4:​7, 8.

Kwa habari zaidi ona sura ya  10 ya kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.