Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Msikiaji wa Sala?

Ni Nani Msikiaji wa Sala?

Ni Nani Msikiaji wa Sala?

IKIWA kuna Msikiaji wa Sala, basi, lazima awe ndiye Muumba. Ni nani mwingine isipokuwa yule aliyeuumba ubongo wa mwanadamu anayeweza kuelewa mawazo yetu? Ni nani mwingine angeweza kusikiliza sala na kuwapa wanadamu msaada wanaohitaji? Huenda ukajiuliza, ‘Je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kuna Muumba? ’

Watu wengi wanafikiri ili mtu aamini kuna Muumba, ni lazima apuuze sayansi ya kisasa. Lakini mawazo ya kwamba Biblia inapingana na sayansi si ya kweli. Fikiria jambo lifuatalo.

▪ Uchunguzi wa hivi karibuni uliohusisha maprofesa 1,646 wa sayansi kutoka vyuo vikuu bora zaidi 21 nchini Marekani ulionyesha kwamba ni asilimia 33 tu waliosema hawaamini kuna Mungu.

Ukweli ni kwamba wanasayansi wengi wanaamini kuna Mungu.

Mambo Yanayothibitisha Kuna Muumba

Je,tunapaswa kuamini kuna Msikiaji wa sala bila kuwa na uthibitisho wowote? Hapana. Wazo la kwamba imani ni kuamini bila uthibitisho wowote si la kweli. Biblia inasema imani ni “uthibitisho ulio wazi wa mambo halisi ingawa hayaonekani.” (Waebrania 11:1) Tafsiri nyingine inasema imani inatusaidia “kusadiki kabisa mambo tusiyoyaona.” (Biblia Habari Njema) Kwa mfano, hatuwezi kuona mawimbi ya redio, lakini sauti unayosikia kupitia redio yako inathibitisha kwamba kuna mawimbi hayo yasiyoonekana, na hivyo unaamini yapo. Vivyo hivyo ingawa hatuwezi kumwona msikiaji wa sala tunaweza kuchunguza uthibitisho na kupata uhakika kwamba kwa kweli yuko.

Tunaweza kupata wapi uthibitisho wa kwamba kuna Mungu? Tunahitaji tu kutazama vitu vinavyotuzunguka. Biblia inasema hivi: “Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Je, unakubaliana na ukweli wa maneno hayo? Huenda unapotafakari jinsi ulimwengu ulivyopangwa kwa utaratibu, chanzo cha uhai, au muundo tata wa ubongo, bila shaka unafikia mkataa wa kwamba ni lazima kuna mtu mwenye uwezo zaidi kuliko wanadamu. *

Lakini hatuwezi kujifunza mengi kumhusu Mungu kwa kutazama tu vitu vinavyotuzunguka. Kuchunguza uumbaji ili kupata uthibitisho wa kuwepo kwa Mungu ni sawa na kusikia hatua za mtu anayetembea nje ukiwa ndani ya nyumba ambayo imefungwa. Unajua kuna mtu nje ya nyumba, lakini ni nani? Ili ujue, unahitaji kufungua mlango. Sisi pia tunahitaji kuchukua hatua kama hiyo ili tumtambue Muumba wa vitu vyote.

Biblia ni mlango unaoongoza kwenye ujuzi kumhusu Mungu. Unapofungua mlango huo na kuchunguza unabii wenye habari nyingi na jinsi ulivyotimia utapata uthibitisho wa kwamba kuna Mungu. * Lakini zaidi ya hayo, kuchunguza jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu kutatusaidia kujua vizuri utu wa Msikiaji wa sala.

Msikiaji wa Sala Ana Sifa Gani?

Biblia inafunua kwamba unaweza kumjua Msikiaji wa sala. Bila shaka, ni lazima Mungu awe na utu wenye sifa fulani ili atusikilize. Ni jambo lenye kutia moyo kusoma hivi: “Ee Msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.” (Zaburi 65:2) Mungu anawasikiliza wale wanaosali kwake kwa imani. Na ana jina. Biblia inasema hivi: “Yehova yuko mbali sana na waovu, lakini huisikiliza sala ya waadilifu.”​—Methali 15:29.

Yehova ana hisia. Yeye ni “Mungu wa upendo” na pia anaitwa “Mungu mwenye furaha.” (2 Wakorintho 13:11; 1 Timotheo 1:11) Kuhusu jinsi alivyohisi wakati uovu ulipokuwa mwingi duniani, Biblia inasema hivi: “Akaumia moyoni mwake.” (Mwanzo 6:​5, 6) Ingawa watu husema Mungu husababisha kuteseka ili kuwajaribu watu, hilo si kweli. Biblia inasema hivi: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu.” (Ayubu 34:10) Hata hivyo, huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Mungu ndiye Muumba mweza-yote, kwa nini ameruhusu wanadamu waendelee kuteseka?’

Yehova amewapa wanadamu uwezo wa kutumia uhuru wa kuchagua, na jambo hilo linatusaidia kujua jinsi Mungu alivyo. Je, hatuthamini uhuru wetu wa kuamua jinsi tutakavyoishi? Lakini kwa kusikitisha, watu wengi wanatumia vibaya uhuru wao na kujisababishia mateso wao wenyewe na wengine pia. Sasa swali la kufikiria kwa uzito ni hili: Mungu ataondoaje kuteseka bila kuwapokonya wanadamu uhuru wao wa kuchagua? Tutachunguza swali hilo katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kwa habari zaidi kuhusu uthibitisho wa kuwapo kwa Mungu ona broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai na kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 10 Broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote na kitabu Biblia​—⁠Neno la Mungu au la Binadamu? kimechapishwa na Mashahidi wa Yehova ili kukusaidia kuchunguza uthibitisho wa kwamba Biblia imeongozwa na roho ya Mungu.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

Inakufanya Uwe na Shaka?

Inasikitisha kwamba dini ndiyo inayofanya watu wengi watilie shaka kwamba kuna Msikiaji wa sala mwenye huruma. Kwa sababu dini imejihusisha na vita, ugaidi, na kutochukua hatua yoyote watoto wanapotendewa vibaya kingono, hilo linafanya hata watu wanaosali waseme, “Siamini kuna Mungu.”

Kwa nini mara nyingi dini imewachochea watu watende mambo mabaya? Kwa ufupi: Watu wengi wamefanya mambo mabaya wakidai ni kwa sababu ya imani yao ya kidini. Biblia ilitabiri kwamba watu waovu wangeingia katika Ukristo na kutenda kinyume cha mapenzi ya Mungu. Mtume Paulo aliwaambia hivi waangalizi Wakristo: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.”​—Matendo 20:29, 30.

Mungu anachukizwa na dini ya uwongo. Kwa kweli, Neno la Mungu, Biblia, linashutumu dini ya uwongo kwa hatia ya kumwaga “damu . . . ya wale wote ambao wameuawa juu ya dunia.” (Ufunuo 18:24) Kwa sababu dini ya uwongo imeshindwa kuwafundisha watu kumhusu Mungu wa kweli ambaye sifa yake kuu ni upendo, dini hizo zina hatia ya damu machoni pa Mungu.​—1 Yohana 4:8.

Msikiaji wa sala anawasikitikia wale wanaoteseka kwa sababu ya kukandamizwa na dini. Hivi karibuni, upendo wa Mungu kuelekea wanadamu utamchochea amtumie Yesu kuwahukumu wanafiki wote wa kidini. Yesu alisema hivi: “Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako?’ . . . Hata hivyo nitawaambia waziwazi: Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.”​—Mathayo 7:22, 23.