Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wakati Wowote Mnaposali, Semeni, ‘BABA’”

“Wakati Wowote Mnaposali, Semeni, ‘BABA’”

“Wakati Wowote Mnaposali, Semeni, ‘BABA’ ”

“Baba.” Neno hilo linafanya ufikirie jambo gani? Mwanamume mwenye upendo na hisia ambaye anahangaikia sana hali ya familia yake? Au mwanamume asiyejali, labda hata anayewatendea wengine vibaya? Maoni yako kuhusu maswali hayo yanategemea sana jinsi baba yako alivyokuwa.

“BABA” ni neno ambalo Yesu alilitumia mara kwa mara alipokuwa akiongea kumhusu Mungu. * Alipowafundisha wafuasi wake kusali, Yesu alisema hivi: “Wakati wowote mnaposali, semeni, Baba.” (Luka 11:2) Lakini Yehova ni baba wa aina gani? Jibu la swali hilo ni muhimu sana. Kwa nini? Kadiri tunavyoelewa Yehova ni baba wa aina gani, ndivyo tutakavyozidi kumkaribia na kumpenda zaidi.

Hakuna mtu anayeweza kutueleza vizuri zaidi kumhusu Baba yetu wa mbinguni isipokuwa Yesu. Alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Baba yake. Yesu alisema hivi: “Hakuna yeyote anayemjua Mwana kabisa ila Baba, wala yeyote hamjui Baba kabisa ila Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Mathayo 11:27) Njia bora kabisa ya kumjua Baba ni kupitia Mwana.

Kupita Yesu, tunaweza kujifunza nini kumhusu Baba yetu wa mbinguni? Fikiria maneno haya ya Yesu: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Maneno hayo ya Yesu yanaonyesha sifa kuu ya Mungu, yaani, Upendo. (1 Yohana 4:8) Yehova anatuonyesha upendo katika njia mbalimbali, kama vile kutupatia kibali chake, kutuonyesha huruma, kutupa ulinzi, kututia nidhamu, na vilevile kwa kutuandalia mahitaji yetu.

Tunahakikishiwa Kupata Kibali cha Baba Yetu

Watoto wanatiwa moyo na kuimarishwa wanapohisi kwamba wazazi wao wanakubaliana na mambo wanayofanya. Hebu wazia jinsi Yesu alivyotiwa moyo aliposikia Baba yake akisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mathayo 3:17) Pia, Yesu anatuhakikishia kwamba Baba anatupenda na anatukubali. Alisema hivi: “Anayenipenda atapendwa na Baba yangu.” (Yohana 14:21) Hayo ni maneno yenye kufariji kama nini! Hata hivyo, kuna mtu ambaye anataka kukunyang’anya faraja hiyo.

Shetani anajaribu kutufanya tutilie shaka ikiwa tuna kibali cha Baba yetu wa mbinguni. Anajaribu kutushawishi tuamini kwamba hatustahili kupata kibali cha Mungu. Mara nyingi, anatokeza hisia hizo tunapokabili matatizo kama vile, ugonjwa, udhaifu, au kuzeeka au tunaposhindwa kutimiza mambo fulani na tunapokabili mambo yanayovunja moyo. Fikiria kisa cha kijana mmoja anayeitwa Lucas, ambaye alihisi hastahili kupata kibali cha Mungu. Lucas anasema kwamba alipokuwa kijana polepole wazazi wake waliacha kufuata mambo ambayo walimfunza. Labda hiyo ndiyo sababu ilikuwa vigumu kwake kuwa na uhusiano mzuri na Baba yake wa mbinguni. Zaidi ya hayo, kwa sababu alikuwa na mwelekeo wa kukosa subira, Lucas alipatwa na matatizo hasa katika uhusiano wake pamoja na wengine. Hata hivyo, pole kwa pole, mke wake mwenye subira na mwenye kumtia moyo​—ambaye Lucas anamwita “baraka ya pekee, zawadi kutoka kwa Mungu”​—alimsaidia kudhibiti mwelekeo wake wa kukosa subira. Baadaye Lucas alitambua kwamba “Kristo Yesu alikuja ulimwenguni ili kuwaokoa watenda-dhambi.” (1 Timotheo 1:15) Lucas anasema kwamba kutafakari kuhusu upendo wa Mungu na kibali chake kumemfanya awe na furaha na kutosheka.

Ikiwa nyakati nyingine unashuku kama Yehova anaweza kukupenda au kukupa kibali, huenda ukatiwa moyo kwa kusoma na kutafakari andiko la Waroma 8:​31-39. Katika andiko hilo mtume Paulo anatuhakikishia kwa upendo kwamba hakuna kitu kinachoweza “kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” *

Baba Mwenye Huruma Nyororo

Baba yetu wa mbinguni anaumia tunapoteseka. Yeye ni Mungu mwenye “huruma nyororo.” (Luka 1:78) Kwa kumwiga Baba yake, Yesu aliwatendea wanadamu wasio wakamilifu kwa huruma. (Marko 1:​40-42; 6:​30-34) Wakristo wa kweli wanajitahidi pia kuiga huruma za Baba yao wa mbinguni. Wanatii himizo la Biblia la kuwa ‘wenye fadhili wao kwa wao, na wenye huruma nyororo.’​—Waefeso 4:32.

Fikiria kisa cha mwanamume anayeitwa Felipe. Siku moja, alipokuwa akielekea kazini, kwa ghafula alihisi maumivu makali, ni kana kwamba alikuwa amedungwa kisu mgongoni. Alikimbizwa hospitalini. Baada ya kuchunguzwa kwa saa nane, mwishowe madaktari waligundua kwamba upande wa ndani wa mshipa fulani ulio moyoni (aorta) ulikuwa umepasuka. Walisema angekufa baada ya dakika 25 tu na kwamba hakukuwa na haja ya kumfanyia upasuaji.

Baadhi ya waabudu wenzake walikuwepo, na walichukua hatua ya kumsaidia Filipe kwa sababu ya kuchochewa na huruma. Mara moja, walifanya mpango ili apelekwe kwenye hospitali nyingine ambako alifanyiwa upasuaji, na wakakaa naye mpaka upasuaji ulipokamilika. Inafurahisha kwamba Filipe alipona. Anapokumbuka wakati huo, Filipe anathamini kwa sababu waabudu wenzake walimwonea huruma. Lakini anaamini kwamba Baba yake wa mbinguni ndiye aliyewachochea wamwonyeshe huruma. “Ni kana kwamba Mungu, kama baba mwenye upendo, alikuwa amesimama kando yangu ili kuniimarisha,” anasema Filipe. Kwa kweli, mara nyingi Yehova anaonyesha huruma kwa kuwachochea watumishi wake duniani waonyeshe sifa hiyo.

Baba Yetu Anatulinda

Mtoto mdogo anapoona hatari, humkimbilia baba yake ili apate ulinzi. Anajihisi salama akiwa amekumbatiwa na baba yake. Yesu alimtegemea kabisa Yehova akiwa mlinzi. (Mathayo 26:53; Yohana 17:15) Sisi pia tunaweza kupata ulinzi kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni. Leo, Yehova anatuandalia hasa ulinzi wa kiroho. Yaani, anatulinda tusipate madhara ya kiroho kwa kutuandalia mambo tunayohitaji ili tuepuke hatari na kutunza uhusiano wetu pamoja naye. Njia moja anayotuandalia ulinzi ni kupitia mashauri yanayotegemea Biblia. Tunapopokea mashauri kama hayo, ni kana kwamba Yehova anatembea nyuma yetu, na kutuambia: “Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”​—Isaya 30:21.

Fikiria mfano wa Tiago na ndugu zake Fernando na Rafael, ambao walikuwa washiriki wa bendi ya muziki wenye mdundo mzito. Walisisimuka sana walipochaguliwa kucheza kwenye jumba moja maarufu la muziki huko São Paulo, Brazili. Ni kana kwamba walikuwa karibu kufanikiwa. Hata hivyo, mwabudu mwenzao aliwaonya kuhusu hatari za kushirikiana kwa ukaribu na watu ambao hawaheshimu sheria za Mungu maishani. (Methali 13:20) Alikazia shauri hilo linalotegemea Biblia kwa kuwaeleza kuhusu jambo alilojionea. Ndugu yake alikuwa amejihusisha na mwendo mchafu kwa sababu ya kushirikiana na watu wabaya. Tiago na ndugu zake waliamua kuacha kuwa wanamuziki. Wote watatu sasa ni Wakristo na ni watumishi wa wakati wote. Wanaamini kwamba kutii mashauri ya Neno la Mungu kuliwalinda wasiharibu uhusiano wao pamoja na Mungu.

Baba Yetu wa Mbinguni Anatutia Nidhamu

Baba mwenye upendo huwatia nidhamu watoto wake, kwa sababu anataka wawe watu wazuri baadaye. (Waefeso 6:4) Baba kama huyo anaweza kuwa na msimamo imara, lakini si mkatili anapowarekebisha watoto wake. Vivyo hivyo, wakati fulani huenda Baba yetu wa mbinguni akatutia nidhamu. Lakini sikuzote Mungu anatutia nidhamu kwa upendo wala si kwa ukatili. Kama tu Baba yake, Yesu hakuwa mkatili kamwe, hata wanafunzi wake walipochukua muda mrefu kutii alipowarekebisha.​—Mathayo 20:20-28; Luka 22:24-30.

Mfikirie mwanamume anayeitwa Ricardo ambaye alithamini Yehova alipomtia nidhamu kwa upendo. Baba ya Ricardo alimwacha alipokuwa na umri wa miezi saba tu. Alipokuwa kijana, Ricardo alitamani sana kuwa na baba. Alijihusisha na mambo mabaya, na dhamiri yake ikaanza kumsumbua. Alipotambua kwamba maisha yake hayakupatana na viwango vya maadili vya Kikristo, aliamua kuongea na wazee katika kutaniko aliloshirikiana nalo. Wazee walimpa mashauri thabiti yaliyotegemea Biblia lakini kwa upendo. Ricardo alithamini nidhamu hiyo. Lakini aliendelea kuteseka sana kwa sababu ya mambo aliyofanya. Alikosa usingizi, akalia, na kushuka moyo. Mwishowe, alitambua kwamba bado Yehova alikuwa anampenda ndiyo sababu akamtia nidhamu. Ricardo alikumbuka maneno ya andiko la Waebrania 12:6 linalosema: “Kwa maana yeye ambaye Yehova anampenda, humtia nidhamu.”

Tunapaswa kukumbuka kwamba nidhamu inamaanisha mengi zaidi ya kuadhibu au kumkaripia mtu aliyekosea. Biblia pia inahusianisha nidhamu na mazoezi. Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni anaweza kutuadhibu kwa kuruhusu tuteseke kwa muda kwa sababu ya makosa yetu. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba nidhamu yake ni mazoezi yanayotusaidia kuishi maisha ya uadilifu. (Waebrania 12:7, 11) Ndiyo, Baba yetu anahangaikia sana hali yetu na anaturekebisha kwa faida yetu.

Baba Yetu Anatuandalia Mahitaji Yetu ya Kimwili

Baba mwenye upendo anajitahidi kuandalia familia yake mahitaji ya kimwili. Yehova yuko hivyo pia. “Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote,” akasema Yesu. (Mathayo 6:25-34) Yehova anaahidi hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”​—Waebrania 13:5.

Mwanamke anayeitwa Nice alitambua ukweli wa maneno hayo mume wake alipofutwa kazi. Mwanamke huyo alikuwa ameacha kazi yenye mshahara mzuri ili atumie wakati mwingi zaidi kuwasaidia wasichana wake wawili na amtumikie Mungu. Sasa wangepataje riziki? Alisali kwa Yehova. Siku iliyofuata, mume wake alienda mahali pake pa kazi ili achukue vitu vyake. Alishangaa mkubwa wake alipomwambia kwamba kulikuwa na nafasi mpya ya kazi na akampa kazi hiyo! Hivyo mume wa Nice alifutwa kazi siku moja, na akapata kazi tena siku iliyofuata. Nice na mume wake walimshukuru Yehova kwa sababu ya matokeo hayo mazuri. Jambo lililowapata linatukumbusha kwamba akiwa Mwandalizi wetu mwenye upendo, Yehova hawasahau kamwe watumishi wake waaminifu.

Kuthamini Upendo wa Baba Yetu

Kwa kweli, maneno hayatoshi kufafanua upendo mwingi wa Baba yetu wa mbinguni! Tunapochunguza njia mbalimbali anazoonyesha upendo wake akiwa baba, yaani, kwa kutuonyesha kibali, huruma, kutulinda, na kututia nidhamu, vilevile kutuandalia mahitaji yetu, kwa kweli tunakata kauli kwamba yeye ndiye Baba bora zaidi!

Tunawezaje kuonyesha kwamba tunathamini upendo ambao Baba yetu wa mbinguni ametuonyesha? Kwa kujitahidi kujifunza mengi kumhusu na makusudi yake. (Yohana 17:3) Kwa kuishi kulingana na amri zake na kufanya mapenzi yake. (1 Yohana 5:3) Kwa kuiga upendo wake tunaposhughulika na wengine. (1 Yohana 4:11) Tukifanya hivyo, tunaweza kuonyesha kwamba tunamwona Yehova kama Baba yetu na kwamba ni pendeleo kuwa watoto wake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Mara nyingi Maandiko yanamtaja Yehova kuwa Baba. Kwa mfano, tunasoma kumhusu Yesu akitumia neno “Baba” karibu mara 65 katika vitabu vitatu vya kwanza vya Injili na zaidi ya mara 100 katika Injili ya Yohana. Pia, Paulo anamwita Mungu “Baba” zaidi ya mara 40 katika barua zake. Yehova ni Baba katika maana ya kwamba ndiye Chanzo cha uhai wetu.

^ fu. 9 Ona sura ya 24, yenye kichwa “Hakuna Kitu Kinachoweza ‘Kututenga na Upendo wa Mungu’” katika kitabu Mkaribie Yehova, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Kadiri tunavyoelewa Yehova ni baba wa aina gani, ndivyo tutakavyozidi kumkaribia na kumpenda zaidi

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Tunaweza kuonyesha kwamba tunamwona Yehova kama Baba yetu na kwamba ni pendeleo kuwa watoto wake

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

YEHOVA ANAONYESHA SIFA ZAKE AKIWA BABA KWA NJIA MBALIMBALI

KIBALI

HURUMA

ULINZI

NIDHAMU

MAHITAJI YA KIMWILI